1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Urusi yasema IS ilihusika na shambulizi la Moscow

Admin.WagnerD24 Mei 2024

Kwa mara ya kwanza Urusi imelitaja kundi linalojiita Dola la Kiislam IS kuhusika na shambulio lilitokoea mnamo Machi 22 kwenye jumba la tamasha huko Moscow.

https://p.dw.com/p/4gEgX
Urusi | Crocus City Hall
Mwonekano wa Jumba la Crocus baada ya shambulio.Picha: Maxim Shemetov/REUTERS

Shambulio ambalo linatajiwa kuwa baya zaidi la kigaidi kuwahi kutokea katika miongo miwili iliyopita. Haya yanajiri huku mapigano yakiripotiwa kuongezeka katika eneo la Kharkiv. 

Shirika la habari la Urusi, RIA Navosti limenukuu mkuu wa Idara ya usalama ya Urusi FSB, Alexander Bortnikov, akisema, katika kipindi cha uchunguzi, imebainika kuwa maandalizi, ufadhili, shambulio na kurudi nyuma kwa magaidi viliratibiwa kupitia mtandao na wanachama wa kundi la Khorasan Province (IS-K) tawi la la dola la kiislam linalofanya kazi huko Afghanistan na Pakistan.

Soma pia: Putin: Huenda pia Ukraine ilihusika na shambulizi

Dola la Kiiiislam limedai kuhusika mara kadhaa na shambulio la Machi 22 ambalo liliua zaidi ya watu 140, lakini Moscow imejaribu mara kwa mara kuihusisha Ukraine na mataifa ya Magharibi na shambulio hilo.

Hata hivyo Bortnikov hakutupilia mbali mtazamo wa Ukraine, akisema kwamba baada ya kukamilisha shambulio hilo, magaidi walipokea maagizo ya wazi kuelekea mpaka wa Ukraine, ambapo mipango ya kutekeleza shambulizi ilikuwa tayari imeandaliwa.

Ukraine mara kadhaa ilikanusha kuhusika na shambulizi hilo, ambapo watu wenye silaha walivamia ukumbi wa Crocus City Hall nje kidogo ya jiji la Moscow kabla ya kulitekeza kwa moto jengo hilo.

Soma pia: Ukraine yadungua droni 36 katika mashambulizi ya usiku

Zaidi ya washukiwa kumi wamekamatwa wakiwemo washambuliaji wanne, ambao wote wanatoka katika taifa la Asia ya Kati la Tajikistan, jamhuri masikini ya zamani ya Kisoviet kwenye mpaka wa kaskazini mwa Afghanistan.

Vita vinaendea kufukuta

Ukraine | Vita
Vita vya Urusi dhidi ya Ukraine, wanajeshi pacha "Jose" na "Alex", wakishika doria katika mkoa wa Kharkiv, huko Vovchansk.Picha: Hanna Sokolova-Stekh/DW

 Huku haya yakijiri mkuu wa jeshi la Ukraine Oleksandr Syrsky amesema vikosi vya Urusi "vimekwama" vilipojaribu kuuteka mji wa mpakani wa kaskazini-mashariki wa Vovchansk lakini mapigano upande wa mashariki bado ni makali.

Syrsky amesema baada ya mafanikio ya awali, adui amekwamishwa kabisa katika vita vya mitaani kwa Vovchansk na alipata hasara kubwa katika vitengo vya mashambulizi.

Kulingana na gavana wa eneo hilo Oleg Synegubov, Zaidi ya watu 11,000 wamehamishwa kutoka eneo la Kharkiv tangu Urusi ilipoanza mashambulizi yake mapya wiki mbili zilizopita.

Kwengineko, Mkuu wa Crimea iliyoambatanishwa na rasi ya Urusi amesema watu wawili wameuwawa katika shambulio la kombora la Ukraine karibu na Simferopol, kituo kikuu cha utawala cha rasi hiyo.

Kupitia mtandao wa kijamii wa Telegraph Sergei Aksyonov, amedokeza kuwa kombora la Ukraine lilipiga jengo tupu karibu na Alushta Pwani ya Bahari Nyeusi.

Shirika la habari la TASS limenukuu wizara ya ulinzi wa Urusi ikisema kwamba ulinzi wa anga umewadungua makombora matatu yaliyovurumishwa kwenye anga ya Crimea, na kwamba jeshi lilikuwa limeharibu ndege tatu zisizo na rubani za baharini za Ukraine zilielekea peninsula.

Hata hivyo Ukraine haijatoa maoni kuhusu tuhuma hizo.