1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi na Ukraine zajadili bei ya gesi

Admin.WagnerD11 Juni 2014

Mazungumzo kati ya Urusi na Ukraine kuhusu bei ya gesi yameanza tena mjini Brussels, huku Ukraine imekataa punguzo lililotangazwa na Urusi. Waziri mkuu wa Ukraine Arseny Yatsenyuk amesema wanataka mkataba mpya.

https://p.dw.com/p/1CGZy
Mabomba ya mafuta yanayopeleka gesi ya Urusi nchini Ukraine
Mabomba ya mafuta yanayopeleka gesi ya Urusi nchini UkrainePicha: picture-alliance/AP Photo

Punguzo hilo lililokataliwa na Ukraine ni la dola 100 kwa kila mita mraba 1000 za gesi, ambalo lilikuwa limetangazwa na kampuni ya gesi ya Urusi, Gazprom. Tangu Machi mwaka huu Urusi ilipandisha bei ya gesi inayoiuzia Ukraine hadi dola 500 kwa kila mita mraba 1000 za gesi, hiyo ikiwa bei ya juu kabisa kuliko inayolipwa na mteja yeyote barani Ulaya.

Hali kadhalika Urusi imesogeza mbele muda wa mwisho uliowekwa kusimamisha upelekaji wa gesi nchini Ukraine ikiwa bado nchi hiyo itakuwa haijalipa madeni yake. Muda huo ambao ulikuwa jana Jumanne umesogezwa hadi tarehe 16 mwezi huu wa Juni. Mkurugenzi Mkuu wa Gazprom Alexei Miller amesema hatua hiyo imechukuliwa kuyapa msukumo mazungumzo yanayoendelea.

Msimamo ule ule

Hata hivyo punguzo hilo la dola 100 kwa kila mita mraba 1000 za gesi halikupokelewa vyema nchini Ukraine. Akizungumza katika baraza la mawaziri asubuhi ya leo, waziri mkuu wa nchi hiyo Arseny Yatsenyuk amesema, ''Tunafahamu mchezo huu wa Urusi, ambapo punguzo la bei linapangwa na serikali na kisha kuondolewa na serikali hiyo hiyo. Msimamo wetu unabaki pale pale-Tunataka mkataba ubadilishwe''

Kamishna wa Ulaya anayehusika na nishati Guenther Oettinger ambaye anasimamia mazungumzo Kati ya Urusi na Ukraine
Kamishna wa Ulaya anayehusika na nishati Guenther Oettinger ambaye anasimamia mazungumzo Kati ya Urusi na UkrainePicha: picture-alliance/dpa

Mkataba anaouzungumzia Yatsenyuk ni ule uliotiwa saini baina ya Urusi na Ukraine mwaka 2009, ambao unaiwekea Ukraine kiasi maalum cha gesi inachopaswa kukinunua, bila kujali kama kinaendana na mahitaji yake ya nishati au la.

Mazungumzo yanayozileta Urusi na Ukraine kwenye meza moja ya mazungumzo mjini Brussels yanafadhiliwa na Umoja wa Ulaya. Kamishna wa umoja huo anayehusika na masuala ya nishati Guenther Oettinger ambaye ni mpatanishi katika mazunguzmo hayo, amesema huenda ikachukua muda wa hadi siku 10 kupata muafaka utakaomaliza msuguano kati ya nchi hizo mbili, kuhusu biashara ya gesi kati yao.

Putin aelezea nia njema

Taarifa kutoka Ikulu ya Urusi, Kremlin imesema kuwa rais wa nchi hiyo Vladimir Putin alizungumza na kansela wa Ujerumani Angela Merkel, na kumwambia kuwa angeuhimiza ujumbe wa nchi yake katika mazungumzo hayo kuwa na mtazamo ambao utasaidia kuyafanikisha mazungumzo, na kupata suluhisho linalozingatia maslahi ya kila upande.

Waziri wa nishati wa Urusi Alexander Novak
Waziri wa nishati wa Urusi Alexander NovakPicha: Janek Skarzynski/AFP/Getty Images

Urusi imekuwa ikiahirisha muda wa mwisho wa kuikatia gesi Ukraine tangu mwanzoni mwa mwezi huu wa Machi, baada ya Ukraine kutoa dola milioni 786 kulipia malimbikizo ya gesi iliyoipokea kutoka Urusi miezi iliyopita.

Asilimia 15 ya gesi inayotumiwa na nchi za Ulaya, ambayo inaagizwa kutoka Urusi, hutiririka kwa njia ya mabomba yanayopita nchini Ukraine.

Mwandishi: Daniel Gakuba/AFP/RTRE

Mhariri: Josephat Charo