1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Urusi, Ukraine zaendelea kushambuliana

27 Novemba 2025

Jeshi la Urusi limezidungua droni 118 zilizorushwa na Ukraine usiku wa kuamkia Alhamisi 27.11.2025. Wizara ya Ulinzi ya Urusi imesema droni 52 kati ya hizo ziliulenga mkoa wa Belgorod unaopakana na Ukraine.

https://p.dw.com/p/54Luk
Kharkiv, Ukraine 23.11.2025
Juhudi za kuzima moto baada ya mashambulizi ya Urusi dhidi ya UkrainePicha: Vyacheslav Madiyevskyy/REUTERS

Urusi pia imesema wanajeshi wake wamefanya mashambulizi yaliyoilenga miundombinu ya nishati na uchukuzi nchini Ukraine, wakati Ukraine imejibu kwa kukishambulia kiwanda cha Urusi cha kutengeneza silaha.

Mpango wa amani wa Trump wakosolewa

Mashambulizi ya pande hizo mbili yanajiri wakati wabunge kadhaa wa chama cha Republican wamekosoa vikali namna Rais Donald Trump anavyoushughulikia mpango uliopendekezwa wa kurejesha amani Ukraine.

Wabunge hao wamesema mpango huo wenye vipengele 28 unaipendelea Urusi. Hofu hiyo imechochewa na ripoti ya shirika la habari la Bloomberg  iliyovujisha mazungumzo ya siri Jumanne kati ya mwakilishi wa Trump Steve Witkoff  na msaidizi wa Rais wa Urusi Vladimir Putin, Yuri Ushakov yaliyoashiria kuipendelea Urusi.