1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulaya kuongeza chanjo milioni 200 za corona Afrika

Mohammed Khelef
15 Septemba 2021

Kwenye hotuba yake ya Hali ya Ulaya, Rais wa Kamisheni ya Ulaya, Ursula von der Leyen, alisema wangelilisaidia bara la Afrika kupata dozi nyengine milioni 200 za chanjo za virusi vya corona.

https://p.dw.com/p/40Lse
Frankreich | Ursula von der Leyen spricht im EU Parlament
Picha: Yves Herman/REUTERS

Kutoka mabadiliko ya tabia nchi na janga la COVID-19 hadi mzozo wa uhamiaji na wa mshikamano miongoni mwa mataifa 27 wanachama wa Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen alitumia hotuba yake hii ya pili bungeni kujenga msimamo na muelekeo mpya wa Ulaya hata kwa masuala ambayo yalikuwepo tangu mara ya mwisho alipotowa hotuba kama hii. 

Kwenye suala tete la mabadiliko ya tabianchi, von der Leyen aliahidi kuzisaidia nchi masikini kupambana na athari na pia kujuwa namna ya kuishi nazo, akiitolea wito Marekani nayo kuchukuwa hatua muafaka.

"Sasa tutapendekeza euro nyengine bilioni nne kwa ufadhili wa masuala ya mabadiliko ya tabianchi hadi kufikia mwaka 2027. Lakini tunaitarajia Marekani pamoja na washirika wetu wengine nao kuchukuwa hatua pia. Hili ni muhimu kwa kuwa kwa kuliziba pengo la kifedha kwenye hili, Marekani na Umoja wa Ulaya zitakuwa zimetowa ishara madhubuti ya kutwaa uongozi wa dunia kwenye mabadiliko ya tabianchi," alisema mkuu wa huyo wa Umoja wa Ulaya mbele ya wabunge mjini Strasbourg, Ufaransa.

Janga la COVID-19

Senegal Coronavirus l Flughafen von Dakar, Covax, Impfdosen
Msaada wa COVAX unaowasilishwa barani Afrika.Picha: John Wessels/AFP/Getty Images

Suala jengine muhimu ni mchango wa Umoja wa Ulaya kwenye vita dhidi ya janga la corona, ambapo Ursula von der Leyen aliahidi kuwa mataifa masikini ya Afrika yangelisaidiwa dozi nyengine milioni 200 za chanjo kukabiliana na janga hilo. 

Msaada huo utakuwa umeshawasilishwa kwa ukamilifu wake kufikia katikati ya mwaka ujao, ikiwa ni nyongeza ya dozi nyengine milioni 250 ambazo tayari zilishaadiwa kutolewa na Umoja wa Ulaya kwa Afrika.

Von der Leyen alisema mbali ya kutowa dola milioni 700 kwa mataifa ya Ulaya, Umoja wa Ulaya tayawri umeshatuma dozi hizo kwa mataifa 130 duniani, akiuita msaada huo kuwa ni "uwekezaji kwenye mshikamano na pia uwekezaji kwenye afya ya ulimwengu."

"Waheshimiwa wabunge, jana hili ni mbio za riadha, sio mchezo wa kuchupa. Tunafuata sayansi. Tunawasilisha kwa Ulaya. Tunawasilisha kwa sehemu nyengine za dunia. Tulifanya hivyo kwa njia sahihi kwa sababu tulifanya kwa njia ya Kiulaya na nafikiri ilifanya kazi," alisema von der Leyen.

Msaada kwa Afghanistan

Deutschland Kaiserslautern | Flüchtlinge aus Afghanistan, Rhine Ordnance Barracks
Majeshi ya nchi za Magharibi kabla hawajamaliza kuondoka Afghanistan.Picha: Sascha Schuermann/Getty Images

Katika hatua nyengine, Rais huyo wa Kamisheni ya Ulaya ameahidi kuongeza msaada wa kibinaadamu kwa Afghanistan na pia kusimama na watu wa taifa hilo, ambalo limeangukia tena mikononi mwa utawala wa Taliban, uliovamiwa na kuangushwa miaka 20 iliyopita na majeshi ya Marekani na washirika wake wa Kimagharibi.

Umoja wa Ulaya umesema utaongeza euro milioni 100 kwenye jumla ya euro milioni 200 ambazo tayari zilishatolewa mwaka huu kwa ajili ya kusaidia miradi ya maendeleo na uwezeshaji raia masikini, hasa wanawake na wasichana.

Hata hivyo, Umoja huo umesema hakuna msaada wowote utakaokwenda mikononi mwa Taliban na umewataka watawala hao wapya wa Afghanistan kuhakikisha wafanyakazi wa huduma za kibinaadamu wanarahusiwa kufanya shughuli zao kwa uhuru na usalama.