1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Sheria na Haki

Ukeketaji wa kitabibu watishia mafanikio yaliofikiwa Afrika

12 Desemba 2023

Kenya ilipopiga marufuku ukeketaji mwaka wa 2011, wachache walitarajia kwamba mila hiyo ilikuwa ikifanyika hadharani kwa sherehe ingehamia kwenye vyumba vya siri, huku wahudumu wa afya wakifanya utaratibu huo kwa siri.

https://p.dw.com/p/4a5Ps
Haki | Maandamano ya wanaharakati wakipinga mila ya ukeketaji
Wanaharakati wakipinga ukeketaji dhidi ya wasichana na wanawakePicha: Marco Longari/AFP/Getty Images

Ukeketaji wa kitabibu kama unavyojulikana unatetewa na watendaji na jamii kama njia "salama" ya kuhifadhi mila, licha ya hatari kwa afya ya mhasiriwa kimwili, kisaikolojia na kingono.

Kulingana na ripoti ya mwaka 2021 ya shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia watoto na wanawake UNICEF, ukeketaji wa kitabibu unazidi kuongezeka nchini Misri, Sudan, Guinea na Kenya, ambapo unatishia kutengua maendeleo yaliyofikiwa na taifa hilo la Afrika Mashariki katika kukomesha mila hiyo, ambayo inahusisha kuondolewa kwa sehemu au kabisa kwa uke.

Kenya inakadiria kuwa viwango vya ukeketaji vilipungua kwa zaidi ya nusu kutoka asilimia 38 mwaka 1998 hadi asilimia 15 mwaka wa 2022. Hata hivyo, wanaharakati wanaonya kuwa takwimu halisi huenda zikawa kubwa zaidi.

Wakati Edinah Nyasuguta Omwenga akipigania maisha yake baada ya kupata matatizo wakati wa kujifungua, aliwasikia madaktari katika hospitali ya Kenya wakielezea hali yake kama mfano wa ukeketaji wenye madhara makubwa yanayoweza hata kusababisha mauti.

Lakini tofauti na maelfu ya wasichana kote Afrika Mashariki, Omwenga alifanyiwa ukeketeji katika hospitali, mikononi mwa muhudumu wa afya, mtindo ambao sasa ni sehemu unaotia wasiwasi kuweka hai mila hiyo haramu.

Soma pia:Jitihada za Tanzania kutokomeza ukeketaji

Katika kaunti ya Kisii, kilomita 300 magharibi mwa Nairobi, zaidi ya asilimia 80 ya taratibu za ukeketaji hufanywa na wahudumu wa afya, kulingana na takwimu za serikali.

Akizungumza na shirika la habari la AFP, Doris Kemunto Onsomu kwa miaka mingi amekuwa akiwakeketa wasichana wanafunziwa shule katika eneo hilo la milimani, akiamini kuwa ni njia mbadala na salama, kuliko utaratibu wa kitamaduni aliopitia akiwa mwanamwali.

Kemunto ambaye ni muhudumu wa afya amesema kwa sababu anajua hatari ya maambukizi, amekuwa akitumia wembe mpya kila wakati, kwa dhana kwamba anasaidia jamii.

Ukeketaji licha ya kuwa ni mila nyuma ya pazia ni biashara

Shughuli hiyo ya ukeketaji wa kisasa ilikuza kipato cha kwa asilimia 50 kila mwezi, kwani alipata wateja kutoka watu wa tabaka la kipacho cha chini na hata matajiri kabla ya kuamua kuiacha.

Afya | Kifaa kinachotumika kukeketa wasichana na wanawake kwa njia ya kienyeji
Mwanamke akionesha moja ya kifaa kinachotumika kukeketa wasichana na wanawakePicha: Yasuyoshi Chiba/AFP/Getty Images

Tina ambaye si jina lake halisi binti wa mhandisi, alikeketwwa nyumbani kwa nyanyake huko Kisii ambako muhudumu wa afya alifika usiku sana na kumfanyia upasuaji mtoto huyo wa miaka minane pamoja na binamu yake.

Binti huyo anasema wakati wa zoezi hilo alihisi kama dunia inaisha, na alihisi maumivu makalina kwamba kwa amri ya nyanyake, aliambiwa alipaswa kubaki peke yake hadi kidonda kitakapo pona.

Sasa mwanafunzi ni katika Chuo Kikuu cha Nairobi, mwenye umri wa miaka 20 anafanya kampeni dhidi ya mila hiyo, akionyesha msukumo unaokua wa waathiriwa wa ukeketaji wa kutokomeza mila hiyo.

Soma pia:Wasichana 700 waokolewa dhidi ya ukeketaji Tanzania

Imani hiyo pia inaendelea kimataifa, na familia zinakiuka sheria za mataifa wanayoishi na kusafiri hadi Kenya kwa utaratibu huo.

Mnamo Oktoba mwaka huu, mahakama ya London ilimtia hatiani mwanamke wa Uingereza kwa kumpeleka msichana wa miaka mitatu katika kliniki ya Kenya ili kufanyiwa ukeketaji wa kimatibabu.

Rais William Ruto amewataka Wakenya kuacha utamaduni wa ukeketaji, lakini wanaharakati wanasema mamlaka inapaswa kuchukua hatua kali zaidi dhidi ya wahusika wakiwemo wahudumu wa afya na familia za waathiriwa.

Juhudi za kukomesha ukeketaji wasichana na wanawake