1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania yataka ulinzi imara katika mpaka wake na Burundi

Prosper Kwigize30 Julai 2018

Kassim Majaliwa ambaye ni waziri mkuu wa Tanzania amevitaka vyombo vya ulinzi kuimarisha ulinzi na usalama katika mpaka wa Tanzania na Burundi ili kuzuia wahamiaji na silaha zinazoingizwa kinyume na sheria

https://p.dw.com/p/32Kcp
Tansania Vizepräsident Kassim Majaliwa
Picha: DW/S. Khamis

Waziri mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuimarisha ulinzi na usalama kuimarisha ulinzi katika mpaka wa Tanzania na Burundi ili kudhibiti uingiaji wa Silaha na wahamiaji haramu.

Agizo hilo amelitoa katika mkutano na watumishi wa Umma, vyombo vya dola na wananchi katika wilaya ya Buhigwe mkoani Kigoma Waziri mkuu Majaliwa amesisitiza kuwa pamoja na mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Tanzania na Burundi lazima taratibu za uingiaji na utokaji wa wananchi wa pande zote mbili uratibiwe na vyombo vya ulinzi.

Bw. Majaliwa ameeleza kuwa kutokana na Tanzania kupakana na nchi zenye migogoro ya kisiasa na kiusalama, vyombo vya ulinzi na usalama hawana budi kushirikiana na wananchi kuhakikisha usalama katika eneo la mpaka wa nchi ya Burundi na Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo DRC yanalindwa

Kuhusu suala la uingiaji wa silaha pamoja na matukio ya uhalifu Majaliwa ameitaja Tanzania kuwa katika kundi la nchi zinazokabiliwa na umiliki haramu wa silaha za kivita ambazo zisipodhibitiwa ipo hatari kwa wananchi kuishi katika mazingira ya hofu na kushindwa kufanya kazi za uzalishaji mali.

Awali akikaribisha msafara wa Waziri mkuu katika eneo la Manyovu mkoanii Kigoma, mkuu wa wilaya ya Buhigwe Brigedia Jenerali Marco Gaguti amebainisha kuwa eneo hilo wamekuwa wakiingia raia kutoka nchi jirani bila kufuata taratibu na kwamba zaidi ya wahamiaji wasio na vibali 1300 walioingia kinyume cha sheria za uhamiaji wamekamatwa katika kipindi cha Januari hadi June mwaka huu pekee.

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Manyovu lililoko mpakani mwa Tanzania na Burundi Bw. Albert Ntabaliba aliutumia mkutano huo kulalamikia kuwepo mbinyo wa vyombo vya usalama hususani Jeshi la Polisi kuzuia ufanyaji wa biashara kati ya Burundi na Tanzania

Waziri mkuu Kassim Majaliwa yuko mkoani Kigoma kwa shughuli za kiserikali ambapo pamoja na mambo mengine amekagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo hususani kilimo cha michikichi na kahawa.

Mwandishi: Prosper Kwigize
Mhariri:Yusuf Saumu

Baadhi ya wahamiaji wa Burundi walioko Tanzania
Baadhi ya wahamiaji wa Burundi walioko TanzaniaPicha: Getty Images/AFP/D. Hayduk