1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwenyekiti wa CHADEMA Mbowe ana kesi ya kujibu

18 Februari 2022

Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi nchini Tanzania imemkuta mwenyekiti wa chama cha upinzani nchini humo Chadema, Freeman Mbowe pamoja na wenzake watatu wana kesi ya kujibu

https://p.dw.com/p/47F85
Tansania Dar es Salaam Freeman Mbowe Oppositionspartei Chadema
Picha: Eric Boniface/DW

Mbowe pamoja na washtakiwa wengine watatu sasa wataanza kupanda kizimbani kuyakabili mashtaka yao na kulingana na wakili wao, washtakiwa hao wamepanga kuwaleta mahakani hapo mashahidi kadhaa. Uamuzi huo wa mahakama umepokelewa kwa hisia mseto huku chama chake kikisema kitatoa msimamo wake baadaye hii leo.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema upande wa Zanzibar, Salum Mwalimu ameiambia DW kuwa kutokana na ukubwa wa shauri hilo na kwa namna lilivyovutia hisia za wengi, msimamo huo utatolewa makao makuu ya chama mbele ya wafuasi wake waliosafiri kutoka kona mbalimbali za nchi.

Tansania Dar es Salaam Anhänger Oppositionspartei Chadema
Wafuasi wa CHADEMA wakiimba nyimbo za kudai hakiPicha: Eric Boniface/DW

Huku kukiwa na ulinzi mkali ulioimarishwa kuanzia askari wenye silaha za moto mpaka makachero waliovalia kiraia, eneo la mahakama lilifurika umati wa wafuasi wa chama cha Chadema, huku baadhi yao wakiwa wamevalia sare za chama chao zikiwa na ujumbe wa aina mbalimbali.

Nje ya ukumbi wa mahakama Mbowe alisindikizwa kuelekea kwenye karandinga na magereza kwa shangwe na nyimbo za wafuasi wake walionekana kutovunjika moyo juu ya yale yanayoendelea.

Lakini baadhi ya kina mama walionekana kumwaga machozi, huku wengine wakielezea hisia zao kutokana na uamuzi huo wa mahakama.

Kesi ya Mbowe aliyekamatwa kwa mara ya kwanza mkoani Mwanza wakati akiwa katika moja ya mikutano ya vuguvugu la kudai katiba mpya, imekuwa ikivuta hisia za wengi ndani nan je na hii leo kundi la wanadiplomasia wa nchi za Magharibi walifika mahakamani hapo kama sehemu ya mashuhuda.

George Njogopa, DW Dar es Salaam