1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel akabidhiwa tuzo ya UN kwa kuwakarimu wakimbizi

Iddi Ssessanga
11 Oktoba 2022

Kansela wa zamani wa Ujerumani Angela Merkel amewahimiza viongozi kuacha kuwafukuza watu kurudi katika mataifa wanakokabiliwa na ukandamizaji wakati akikubali tuzo ya heshima ya Nansen inayotolewa na UNHCR.

https://p.dw.com/p/4I1xN
Schweiz Angela Merkel erhält den UNHCR Nansen Refugee Award
Picha: Stefan Wermuth/ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Merkel, aliyesifiwa kwa kujitolea kwake alikoonyesha akiwa madarakani kulinda watu waliokimbia makazi yao kutokana na migogoro, alisisitiza "haki za wakimbizi lazima ziheshimiwe".

"Hakuna mkimbizi anayepaswa kurejeshwa katika nchi zao ambako wanakabiliwa na mateso," alisema wakati wa hafla ya kukabidhiwa tuzo ya kifahari mjini Geneva.

Kamati ya uteuzi ya UNHCR ilimtambua Merkel kwa "uongozi, ujasiri na huruma" wakati Ujerumani ilipokaribisha zaidi ya wakimbizi na waomba hifadhi milioni 1.2 mwaka 2015 na 2016 katika kilele cha mzozo wa uhamiaji barani Ulaya uliochochewa hasa na vita nchini Syria.

Wakati huo, Merkel ambaye wakati huo alikuwa kansela alisema hali hiyo "iliyaweka majaribuni maadili yetu ya Ulaya kuliko wakati wowote ule. Ulikuwa uamuzi wa kibinadamu".

Urathi wa Merkel

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi limeangazia jinsi alivyotoa wito kwa Wajerumani wenzake kukataa utaifa unaoleta migawanyiko, na kuwataka badala yake wawe na "huruma na wawazi".

Soma pia: Merkel atetea urathi wake wa Urusi, asema hataomba radhi

Akimkabidhi tuzo ya dhahabu ya Nansen, mkuu wa shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa Filippo Grandi amesema Merkel ameonyesha "maono, ujasiri na ujasiri".

Schweiz Angela Merkel erhält den UNHCR Nansen Refugee Award
Mkuu wa shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR, Filipo Grandi akimkabidhi tuzo ya Nansen, kansela wa zamani wa Ujerumani Angela Merkel jini Geneva, Oktoba 10,2022, kutokana na mchango wake kuwakaribisha wakimbizi.Picha: Stefan Wermuth/ASSOCIATED PRESS/picture alliance

"Ulionyesha dira ya maadili, ambayo sio tu iliongoza kazi yako na matendo ya nchi yako, lakini ilionyesha njia kwa wengi wetu Ulaya na duniani," alisema.

Wakati ambapo idadi ya watu waliolaazimishwa kukimbia makazi yao duniani imepindukia milioni 100 kwa mara ya kwanza, Grandi alimwambia Merkel: "Mfano wako ni na lazima uwe mfano kwa viongozi wengine."

Akikubali tuzo hiyo mbele ya takriban watu 500, Merkel, akiwa amevalia koti jekundu la suti, alikiri kwamba Ujerumani ilikuwa imekabiliwa na "changamoto kubwa" baada ya wakimbizi wengi kuwasili mara moja.

Soma pia: Miaka mitano tangu maelfu ya wakimbizi walipoingia Ujerumani

Lakini mwanamke huyo ambaye wakati huo aliwaambia Wajerumani kauli maarufu: "Wir shaffen das", au "Tunaweza", alisema alijivunia kuwa wamemthibitisha kuwa sahihi.

"Natumai mifano mizuri itaenea na ninatumai katika siku zijazo watu wengi zaidi watahisi kuwajibika kutoa hifadhi kwa watu wengine wanaohitaji," alisema. "Hakuna mtu anayeacha nchi yake kwa hiari na bila kuzingatia kwa uangalifu."

Nini amefanya Merkel na pesa za zawadi?

Wakati akikubali tuzo yake, Merkel alisema angependelea pesa zake za tuzo hiyo ambazo ni kiasi cha dola za Marekani 150,000 zigawiwe miongoni mwa washindi wanne wa kikanda, mbali ya zawadi zao za dola 50,000.

Washindi wa kikanda ni pamoja na Nagham Hasan, daktari wa magonjwa ya wanawake wa Iraq anayetoa huduma ya matibabu na kisaikolojia kwa wasichana na wanawake wa Yazidi ambao walinusurika utumwa, ubakaji na unyanyasaji mwingine mikononi mwa vikundi vya itikadi kali kaskazini mwa Iraqi.

Soma pia: Ujerumani yaonya kuhusu wimbi kubwa la wakimbizi

Mshindi mwingine ni Vincenta Gonzalez, ambaye alianzisha ushirika wa kakao nchini Costa Rica kusaidia wakimbizi, Kikosi cha Zimamoto cha Mbera -- kikundi cha kuzima moto cha wakimbizi wa kujitolea nchini Mauritania -- na Meikswe Myanmar, kikundi cha kibinadamu kinachosaidia wakimbizi wa ndani. nchi yenye migogoro.

Tuzo ya kila mwaka ya Nansen iliundwa mwaka wa 1954 kwa heshima ya Kamishna Mkuu wa kwanza wa Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa, Mvumbuzi wa Arctic wa Norway na mtaalamu wa kibinadamu Fridtjof Nansen, kuashiria kazi bora kwa niaba ya wakimbizi.

Chanzo: AFP