1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIsrael

Jamii ya kimataifa yalaani machafuko ya Al-Aqsa Jerusalem

5 Aprili 2023

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amesema nchi yake inafanya juhudi kutuliza hali kufuatia makabiliano kati ya polisi na waumini katika msikiti wa Al-Aqsa mjini Jerusalem.

https://p.dw.com/p/4Pjyf
Israel | Die Zusammenstöße in Jerusalem
Picha: AHMAD GHARABLI/AFP/Getty Images

Kupitia taarifa, Benjamin Netanyahu amesema Israel imejitolea kuhakikisha uhuru wa kuabudu, uhuru wa kuwepo kwa dini zote na madhehebu yote. Na kwamba hawataruhusu watu wenye misimamo mikali kubadili hilo,"

Alisisitiza kuwa amejitolea kuheshimu makubaliano ambayo yamekuwepo kwa muda mrefu sasa kuhusu eneo la msikiti huo.

Netanyahu aliwaita waumini waliojifunika nyuso na kujifungia msikitini humo kuwa wenye misimamo mikali waliowazuia Waislamu kuingia kwenye eneo hilo la ibada kwa amani.

Vurugu zazuka, polisi wa Israel waingia msikiti wa Al-Aqsa

Kwingineko Jumuiya ya nchi za kiarabu ilishutumu uvamizi huo uliofanywa na polisi ya Israel mapema Jumatano katika msikiti wa Al-Aqsa. Jumuiya hiyo imesema itafanya mkutano baadaye leo kuhusu vurugu hizo. Mkutano huo uliitishwa na Jordan kwa ushirikiano na Misri na maafisa wa Palestina.

Mjumbe wa UN Mashariki ya Kati asikitishwa na machafuko ya Al-Aqsa

Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa katika Mashariki ya Kati Tor Wennesland amesema, amesikitishwa na picha za machafuko katika msikiti huo. Ameshutumu ukamataji wa watu wengi na vilevile ripoti kwamba Wapalestina wanahifadhi makombora na mawe.

Benjamin Netyanyahu, Waziri Mkuu wa israel
Benjamin Netyanyahu, Waziri Mkuu wa israelPicha: Ronen Zvulun/REUTERS

Ujerumani imetoa wito kwa pande zote kuepusha machafuko zaidi katika eneo hilo.

Mvutano mkali waibuka Umoja wa Mataifa juu ya ziara ya Al-Aqsa

Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani amesema kila mtu ambaye ana ushawishi kuhusiana na hali hiyo anapaswa kuwajibika asije akapalia makaa moto, badala yake afanye kila juhudi kutuliza hali.

Ameongeza kuwa wanalaani mashambulizi ya makombora kutoka Gaza kueleka Israel, na kwamba Ujerumani ina wasiwasi kuhusu machafuko hayo.

Jumuiya ya Kiarabu kuandaa mkutano kuhusu vurugu za Al-Aqsa

Uturuki vilevile imeshutumu ghasia hizo na kusema hazikubaliki na kwamba zimekiuka hadhi ya utakatifu wa msikiti huo.Baraza la Usalama lakutana kuhusu mzozo wa Palestina

Akizungumza pembezoni mwa mkutano wa Jumuiya ya kujihami ya NATO mjini Brussels, waziri wa mambo ya nje wa Uturuki Mevlut Cavusoglu amesema juhudi za kurejesha uhusiano wa kawaida na Israel zimeanza lakini ha,ziwezi kufanyika kwa gharama ya misimamo yao kuhusu Palestina. Ameongeza kuwa mashambulizi hayo yamepitiliza.

Kwa muda mrefu, eneo la msikiti wa Al-Aqsa limekuwa kitovu cha mvutano kati ya vikosi vya usalama vya Israel na Wapalestina.
Kwa muda mrefu, eneo la msikiti wa Al-Aqsa limekuwa kitovu cha mvutano kati ya vikosi vya usalama vya Israel na Wapalestina.Picha: Ammar Awad/REUTERS

 

Palestina yalaani ziara ya waziri wa Israel eneo la Al-Aqsa

Mapema Jumatano, polisi ya Israel ilivamia msikiti wa Al-Aqsa, ili kuwafurusha watu iliowaita kuwa wachochezi. Polisi hao waliwakamata zaidi ya watu 350.

Kulingana na Polisi ya Israel maafisa wake walilazimika kuingia msikitini humo baada ya vijana kadhaa waliokuwa wakivunja sheria na waliojifunga barakoa usoni kujifungia ndani ya msikiti huo.

Wanamgambo wa Palestina walijibu uvamizi huo wa polisi wa Israel kwa kufyatua makombora kuelekea Israel kutoka ukanda wa Gaza, unaodhibitiwa na Hamas.

Hatua iliyosababisha Israel kujibu kwa mashambulizi ya angani.

(Vyanzo: APE, AFPE, RTRE)