1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China kutuma dola milioni 14.7 kusaidia Venezuela

29 Juni 2026

Wizara ya mambo ya nje ya China imesema nchi hiyo itatuma dola milioni 14.7, kama msaada wa dharura kwa Venezuela, baada ya matetemeko mawili makubwa ya ardhi yaliyosababisha vifo vya watu zaidi ya 1,450.

https://p.dw.com/p/5GFCz
China Peking 2025 | Chinas Außenamtssprecher Guo Jiakun
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya China Guo Jiakun Picha: Johannes Neudecker/dpa/picture alliance

Maelfu ya watu wengine wamejeruhiwa huku zaidi ya 50,000 wakiwa hawajulikani waliko.

Msemaji wa wizara hiyo Guo Jiakun ameuambia mkutano wa waandishi habari kwamba, China itasaidia pia katika ujenzi mpya wa  Venezuela  baada ya janga hilo pamoja na kusaidia kutoa picha za satelaiti za maeneo yaliyoathirika ili kusaidia katika shughuli za uokoaji.

"China ina wasiwasi mkubwa kuhusu janga la tetemeko la ardhi nchini Venezuela. Rais Xi Jinping ametuma salamu zake za rambirambi kwa Rais wa mpito wa Venezuela Delcy Rodríguez. Serikali ya China imeamua kuipatia Venezuela msaada wa ziada wa dola milioni 14.7 ili kusaidia juhudi za uokoaji na ujenzi mpya baada ya maafa. Vifaa vya msaada vitasafirishwa kwenda Venezuela haraka iwezekanavyo.”

Jiakun ameongeza kuwa China itatoa msaada zaidi kwa Venezuela kadri hali itakavyoendelea kubadilika.

Siku ya Jumatano, Venezuela ilipigwa na matetemeko mawili ya ardhi yenye ukubwa wa 7.2 na 7.5 katika kipimo cha Richter na kusababisha maafa na uharibifu mkubwa wa mali na miundombinu.

Raia nane wa China ni miongoni mwa walioangamia katika janga hilo.