1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Cavusoglu aitembelea Saudia tangu mauaji ya Khashoggi

10 Mei 2021

Waziri wa mambo ya nje wa Uturuki anaitembelea Saudi Arabia kwa mara ya kwanza tangu mauaji ya mwandishi wa Saudi Arabia, Jamal Khashoogi 2018, yalipouharibu uhusiano wa nchi hizo, ambao toka hapo ulikuwa wa mashaka.

https://p.dw.com/p/3tCcE
Türkei Mevlut Cavusoglu
Picha: Reuters/Turkish Foreign Ministry

Mevlut Cavusoglu atakuwa mjini Riyadh leo Jumatatu na kesho ambapo atakutana na mwenzake Faisal bin Farhan na kujadili masuala ya uhusiano baina ya mataifa yao pamoja na kubadilishana mawazo kuhusu masuala ya kikanda.

Ziara hiyo ya Cavusoglu inafanyika baada ya wiki iliyopita kufanyika mkutano wa manaibu mawaziri wa mambo ya nje wa Uturuki na Misri uliolenga kutatua mivutano ya muda mrefu baina ya mahasimu hao wa kikanda.

Ulikuwa mkutano wa kwanza wa ngazi hiyo ya juu baina ya nchi hizo tangu mwaka 2013. Uturuki na Saudi Arabia zimekuwa kwenye uhusiano wa mashaka kwa miongo, uliochochewa na uhasama kuhusu kupanda na kushuka kwa kundi la udugu wa kiislamu tangu ziliposhuhudiwa harakati za mwaka 2011 za  kuunga mkono demokrasia.