1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zaidi ya watu 20,400 wauawa Gaza tangu kuanza kwa vita

24 Desemba 2023

Wizara ya Afya inayoongozwa na Hamas imesema leo kwamba takriban watu 20,424 wameuawa katika ardhi ya Palestina tangu kuanza kwa vita kati ya kundi la Hamas na Israel, wengi wao wakiwa wanawake na watoto.

https://p.dw.com/p/4aXl2
Ukanda wa Gaza | Jengo lililoharibiwa na shambulio la Israel Khan Yunis
Jengo lililoharibiwa na shambulio la Israel Khan YunisPicha: SAID KHATIB/AFP/Getty Images

Wizara ya afya inayoongozwa na kundi la Hamas imeongeza kwamba idadi hiyo inajumuisha vifo 166 vilivyotokea katika muda wa saa 24 zilizopita, wakati mapigano yanaendelea kati ya jeshi la Israel na Hamas.

Mzozo wa kibinadamu unashuhudiwa katika ukanda wa Gaza tangu kuanza kwa mapigano hayo ambapo sehemu kubwa ya Gaza imesalia magofu huku takriban wakaazi milioni 2.4 wakikabiliwa na uhaba wa maji, chakula na madawa kutokana na mzingiro wa vikosi vya Israel ambao umetatiza hata kuwasili kwa misaada ya kiutu.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa asilimia 80 ya wakaazi wa Gaza wameyakimbia makaazi yao, huku wengi wao wakilazimishwa kuelekea kusini mwa Gaza.