1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zaidi ya watu 200 wafariki kutokana na mafuriko Afrika

Saleh Mwanamilongo
11 Septemba 2020

Mafuriko yaliyosababishwa na mvua kali yamewauwa watu 200 na kuwaacha wengine zaidi ya milioni moja bila makaazi kuanzia Senegal hadi Sudan kwa mujibu wa takwimu za serikali.

https://p.dw.com/p/3iLr7
Sudan Überschwemmungen
Picha: Reuters/A. Campeanu

Mafuriko yaliyosababishwa na mvua kali yamewauwa watu 200 na kuwaacha wengine zaidi ya milioni moja bila makaazi kuanzia Senegal hadi Sudan kwa mujibu wa takwimu za serikali.

''Tumehesabu watu 760,000 walioathirika na mafuriko na wengine 110 kufariki na mvua bado kumalizika'' kwenye nchi 11 za Afrika ya Kati na Magharibi, alisema Julie Belanger, mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kiutu (OCHA) kwenye kanda hiyo.

Takwimu hizo zinaongezwa kwa hizo za Sudan ambako watu 103 wamekufa na wengine 550,000 kuathirika na mafuriko, kwa mujibu wa shirika la OCHA mjini Karthoum.

''Tunatarajia kuwa na mwaka maalum ambao idadi ya maafa itazidi hiyo ya mwaka 2019'', alielezea Bi Belanger. Amesema shirika la misaada ya dharura la Umoja wa Mataifa linatarajia kutoa msaada ikiwa hali itaendelea kuwa mbaya.

 Mwaka 2019, shirika hilo lilitoa msaada wa dola milioni 29 kwa ajili ya nchi 11, bila kuijumuisha Sudan, zilizoathirika na mafuriko. Mafuriko yamesababisha magonjwa yanayotoka na maji machafu kama vile kipindupindu na malaria.

Watu zaidi ya 100 wamekufa nchini Sudan kutokana na mafuriko.
Watu zaidi ya 100 wamekufa nchini Sudan kutokana na mafuriko.Picha: EBRAHIM HAMID/AFP/Getty Images

Miongoni mwa nchi zilizoathirika sana ni pamoja na Niger ambako watu 71 walikufa na wengine 350,000 kuachwa bila makaazi. Waziri Mkuu wa Niger, Brigi Rafini alitoa mwito wa msaada kufuatia mkutano Ijumaa na mashirika ya misaada ya kimataifa na mabalozi wa nchi za kigeni mjini Niamey.

Shirika la OCHA linaelezea kwamba Niger inahitaji dola milioni 10 kwa ajili ya msaada wa kiutu wa haraka. Nchini Senegal, mji mkuu Dakar umeathirika pia ambako watu sita wamekufa. Nchini Chad watu wapatao 190,000 wameathirika. Na huko Nigeria jimbo la Borno pekee lina watu 26,000 walioathirika na mafuriko hayo kwa mujibu wa shirika la OCHA. Cameroon, Chad na Ghana ni nchi ambazo zimaethirika pia.