1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakorea kusini wakutana na Wakorea kaskazini

Sekione Kitojo
20 Agosti 2018

Wakorea kusini kadhaa wamevuka mpaka wenye ulinzi mkali na kuingia Korea kaskazini Jumatatu na kukutana na ndugu zao ambao wengi hawajaonana kwa muda mrefu tangu nchi hizo kutengana kutokana na mvutano wa vita vya Korea.

https://p.dw.com/p/33Pls
Familienzusammenführungen Nord- und Südkorea
Picha: Reuters/Yonhap

Tukio  hilo litakalodumu kwa  muda  wa  wiki  moja  katika  mji  wa kitalii  ulioko  katika  milima  ya  Diamond  nchini  Korea  kaskazini linakuja  wakati  Korea  hizo  mbili  zinaimarisha  juhudi  za maridhiano huku  kukiwa  na  msukumo  wa  kidiplomasia  kutatua mkwamo  wao  kuhusiana  na   azma  ya  Korea  kaskazini  ya mpango  wake  wa silaha  za  kinyuklia  ambao unaweza kushambulia  bara  la  Amarika.

Familienzusammenführungen Nord- und Südkorea
Wanafamilia wakikutana tena kati ya Korea kusini na kaskaziniPicha: Reuters/Yonhap

Kukutana  huko  kwa  muda  kwa  ndugu  kutoka  pande  hizo  mbili kunaonekana  kuwa  na  hisia  kali  kwasababu  washiriki  wengi  ni wazee  na  wana  haja  ya  kuwaona  wapendwa  wao  kwa  mara nyingine  tena  kabla  hawajafariki.  Familia  nyingi  zimegawika wakati  wa  vita  vya  Korea  vya  mwaka  1950-53, ambavyo vilimalizika  kwa  makubaliano  ya  kusitisha  mapigano , na  sio mkataba  wa  amani, na  kuliacha  eneo  la  rasi  ya  Korea  kiufundi katika  hali  ya  vita.

Mabasi  yaliyowabeba  kiasi  ya  wazee  90 kutoka  Korea  kusini pamoja  na  wanafamilia  wengine  yaliingia  katika  mji  huo  wa kitalii  wa  milima  ya  Diamond  baada  ya  kuvuka  kuingia  nchini Korea  kaskazini. Hapo  mapema  asubuhi,  Wakorea  kusini , baadhi wakiwa  katika viti vya  kusukuma na  wakisaidiwa  na  wafanyakazi wa  shirika  la  msalaba  mwekundu , waliyaacha  mabasi  kwa  muda na  kuingia  katika  ofisi  za  uhamiaji  za  Korea  kusini katika  mji wa  mpakani  wa  mashariki  wa  Goseong.

Walikuwa  wanakutana  tena  leo  mchana na  ndugu  zao  wa Korea kaskazini  ambao  walipoteana  kwa  muda  mrefu  mwanzoni  mwa tukio  hilo  la  siku  tatu. Duru  nyingine  ya  kukutana  kuanzia  Ijumaa hadi  Jumapili  itahusisha  zaidi  ya  Wakorea  kusini 300, kwa mujibu  wa  wizara  ya  muungano  ya  mjini  Seoul.

Familienzusammenführungen Nord- und Südkorea
Wanaonekana wanafamilia wakikumbatiana baada ya kutengana kwa muda mrefuPicha: Reuters/Yonhap

Wakimbizi wa vita

Makutano  yaliyopita  yametoa  picha  nzuri  za  wazee Wakorea wakilia, wakikumbatiana na  kuonesha  mapenzi  makubwa kwa  kila mmoja.  Karibu  watu 20,000 wamekuwa  wakishiriki  katika  duru  20 za  kukutana  uso  kwa  uso  tangu  mwaka  2000.

Wengine 3,700 walibadilishana  ujumbe  wa  vidio  na  ndugu zao  wa Korea  kaskazini chini  ya  mpango  huo  unaodumu  kwa  muda mfupi  kuanzia  mwaka  2005 hadi  2007.

Hakuna  aliyewahi  kupata  nafasi  ya  pili  kuwaona ndugu. Wengi wa  washiriki  kutoka  Korea  kusini  ni  wakimbizi  wa  vita waliozaliwa  nchini Korea kaskazini  ambao  watakutana  na  ndugu zao , ama  watoto  wao  waliokuwa  wadogo  waliobakia  nchini humo, wengi  wao  ambao  sasa  wamo katika  umri  wa  miaka  ya 70.

Park Hong-seo , mwenye  umri  wa  miaka  88  ambaye  alipigana vita  vya  Korea  kutoka  mji  wa  kusini  wa  Daegu, amesema anawaza  kila  mara  iwapo alikabiliana  na  kaka  yake  mkubwa katika  mapambano.

Familienzusammenführungen Nord- und Südkorea
Washiriki wa tukio hilo la kukutana tena wakiteremka katika mabasiPicha: Reuters/Kim Hong-Ji

China yaingilia kati

Baada  ya  kumaliza  masomo  yake  katika  chuo  kikuu cha  mjini Seoul, kaka  yake  Park alikwenda  kuishi  katika  mji  wa  pwani  wa Korea  kaskazini wa Wonsan akifanyakazi  kama  daktari  wa  meno mwaka 1946.

Baada  ya   vita  kuzuka, Park aliambiwa  na  mfanyakazi  mwenzake kuwa  kaka  yake  amekataa  kukimbilia  Korea  kusini kwasababu alikuwa  na  familia  upande  wa  kaskazini  na  ni daktari  katika jeshi  la  Korea  kaskazini.

Park alipigana  upande  wa  Korea  kusini  akiwa  mwanafunzi mwanajeshi  na  alikuwa  miongoni  mwa vikosi vya  muungano ambavyo  viliukamata  mji  wa  Wonsan Oktoba  mwaka  1950. Majeshi  yaliyokuwa  yakiongozwa  na  Marekani  yalisonga mbele zaidi  upande  wa  kaskazini  katika wiki  zilizofuata  kabla  ya kufurushwa  kurejea  nyuma na  majeshi  ya  China baada  ya Beijing  kuingilia  kati  katika  mzozo  huo.

Familienzusammenführungen Nord- und Südkorea
Baadhi ya washiriki wakiwa hata hawawezi kutembea wakiwa katika viti vya magurudumuPicha: Reuters/Kim Hong-Ji

Park  alikuja  kufahamu  kwamba  kaka  yake  alifariki  mwaka  1984. Katika  mlima  Diamond  atakutana  na watoto wa kiume  na  kike  wa kaka yake  kutoka  Korea  kaskazini  ambao sasa  wana  umri  wa miaka 74 na 69.

Mwandishi:  Sekione  Kitojo / ape

Mhariri: Mohammed  Abdul Rahman