1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Venezuela yaishutumu Marekani kwa 'wizi wa waziwazi'

11 Desemba 2025

Serikali ya Venezuela imeituhumu Marekani kwa kile ilichokiita “wizi wa wazi” baada ya Washington kuikamata meli ya mafuta iliyowekewa vikwazo karibu na pwani ya Venezuela.

https://p.dw.com/p/557mW
Venezuela Caracas / Marekani Pittsburgh 2025 | Nicolás Maduro na Donald Trump
Rais wa Marekani Donald Trump alionya mnamo Novemba 29, 2025 kwamba anga ya juu na karibu na Venezuela inapaswa kuzingatiwa kuwa imefungwa, ikiwa ni ongezeko la mzozo na kiongozi wa mrengo wa kushoto Nicolas Maduro.Picha: Juan Barreto/Andrew Caballero-Reynolds/AFP

Katika taarifa yake, serikali ya Venezuela imeeleza kwamba itatetea "uhuru wake, rasilimali zake za asili, na heshima ya kitaifa kwa msimamo mkali kabisa.” Imeongeza kwamba itawasilisha malalamiko yao kwa mashirika ya kimataifa.

Rais wa Marekani Donald Trump alithibitisha kukamatwa kwa meli hiyo mapema jana Jumatano, hatua iliyosababisha bei ya mafuta kupanda na kuongeza mvutano kati ya Washington na Caracas.

Kukamatwa kwa meli hiyo kunakochukuliwa kama juhudi za karibuni za utawala wa Trump kuongeza shinikizo kwa Rais wa Venezuela Nicolas Maduro ambaye ameshtakiwa kwa makosa ya biashara haramu ya dawa za kulevya na ugaidi.

Wavenezuela wagawanyika juu ya hatua za Trump

Wavenezuela katika eneo la Florida Kusini hata hivyo wamegawanyika kuhusiana na hatua zinazofuata za Rais Donald Trump, wakati Marekani ikiendelea kupeleka vikosi zaidi vya kijeshi na kuzishambulia boti kutokea angani

Bahari ya Karibiki nje ya Venezuela 2025 | Helikopta za kijeshi za Marekani zilizohusihwa na kukamata meli za mafuta
Helikopta ya kijeshi ya Marekani ikiruka karibu na meli ya mafuta wakati wa uvamizi ulioelezewa na Mwanasheria Mkuu wa Marekani Pam Bondi kama utekaji wa Marekani nje ya pwani ya Venezuela, Desemba 10, 2025.Picha: U.S. Attorney General/REUTERS

Watu wengi walioko ughaibuni wanatamani kupata kiongozi mpya kuchukua nafasi ya Rais Nicolas Maduro nchini Venezuela, nchi ambayo maelfu wamekimbia kutokana na mgogoro wa kiuchumi na kisiasa katika miaka ya hivi karibuni.

"Ikiwa kuna hisia moja ya kawaida miongoni mwa Wavenezuela wote, ni chuki tuliyo nayo dhidi ya Chavismo na Maduro," alisema Andrea Gonzalez, mwenye umri wa miaka 38, akimaanisha itikadi ya mrengo wa kushoto iliyopewa jina la mtangulizi wa Maduro, marehemu Hugo Chavez.

Tofauti zaibuka kuhusu jinsi ya kumwondoa Maduro

Baadhi wanasema matumizi ya nguvu ndiyo chaguo pekee, hasa baada ya Maduro kujitangaza tena kuwa rais mwaka 2024 katika uchaguzi ambao ulionekana kugubikwa na udanganyifu.

Lakini wengine, wanaohofia uharibifu unaoweza kusababishwa na vita, wanataka kutumia njia za kidiplomasia.

Ingawa utawala wa Trump umesema unawalenga "magaidi wa dawa za kulevya," wengi wanahoji nia ya kweli ya Washington ya kuingia ghafla kijeshi katika nchi hiyo ya Amerika Kusini yenye akiba kubwa ya mafuta duniani.

'Upanga ukatao pande zote'

Maduro kwa muda mrefu amedai kwamba Washington inakusudia kumpindua. Na huko Doral, karibu na Miami, ambapo zaidi ya asilimia 40 ya wakazi wana asili ya Venezuela, Diana Gonzalez anaamini kwamba huo ndio ukweli.

Marekani Doral 2025 | Mkesha wa kurefusha Hadhi ya Muda ya Ulinzi kwa Wavenezuela
Wavenezuela wakiwa na mabango yanayoelezea hali halisi nchini wakati wa mkesha uliofanyika Doral, Florida na Chama cha Wamarekani cha Venezuela kuunga mkono upanuzi wa TPS kwa Wavenezuela waliolazimika kuondoka nchini mwao kutokana na uongozi wa kidikteta wa Nicolas Maduro, Alhamisi, Mei 8, 2025.Picha: Pedro Portal/IMAGO

Mbunifu huyo wa mapambo ya ndani mwenye umri wa miaka 47 anaunga mkono uingiliaji kati wa "asilimia 100" katika nchi yake ili kuipindua serikali anayoituhumu kwa ufisadi, kuvuruga uchaguzi na kuwakandamiza wapinzani.

Baada ya miaka mingi ya majaribio ya amani ambayo hayajafanikiwa, hilo ndilo chaguo pekee linalowezekana, alisema.

"Hatuwezi kuendelea peke yetu kwa sababu ni mapambano yasiyo ya haki kati ya watu waliobeba bendera dhidi ya watu wenye silaha," alisema, akiongeza kwamba "hakuna mtu yeyote nchini Venezuela atakayepigania utawala."

Lakini kwenye eneo hili la Doral, wengi hujiepusha kuzungumzia suala hilo na pia wengine hawapendi kumzungumzia Trump.

Hatua ya serikali ya Trump ya kuwakamata wahamiaji wengi wa asili ya Amerika ya Kusini baada ya kufuta Hadhi ya Ulinzi wa Muda (TPS) iliyotolewa kwa Wavenezuela wapatao 600,000 chini ya utawala wa rais aliyepita Joe Biden imeathiri pakubwa jamii hiyo. Na hilo limesababisha mvutano.

Andrea Gonzalez, anayeunga mkono mipango ya Trump nchini Venezuela lakini anakosoa sera zake za uhamiaji nchini Marekani, baada ya yeye binafsi kupitia kadhia hiyo.

Hata hivyo, anaamini kwamba Trump anaweza kurejesha imani katika jamii yake ikiwa atafanikiwa kumpindua Maduro.