1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Ukraine yarejesha zaidi ya kilometa za mraba 35 za ardhi

3 Julai 2023

Vikosi vya Ukraine vimechukua zaidi ya kilomita za mraba 35 za ardhi katika eneo ambalo linadhibitiwa na vikosi vya Urusi huko Bakhmut mashariki wiki iliyopita. Jeshi la anga leo limedungua ndege 13 kati ya 17 za Urusi.

https://p.dw.com/p/4TLgP
Ukraine Bachmut | Soldat der Wagner Gruppe
Picha: Valentin Sprinchak/TASS/IMAGO

Hivi karibuni vikosi vya Ukraine vilirejesha kilomita za mraba takribani tisa huko Bakhmut ambao ni mji wa kimkakati ulioshuhudia makabiliano makali kati ya vikosi vya Ukraine na Urusi.

 Vile vile, kilomita nyingine za mraba 28.4 katika maeneo mbalimbali ya kusini zimerejeshwa na Ukraine.

Naibu Waziri wa Ulinzi wa Ukraine, Hanna Maliar, amesema wakati vikosi vyake vikiendelea kusonga mbele kukomboa maeneo mengine huko Bakhmut, vikosi vya Urusi vimeendeleza mashambulizi katika maeneo ya Lyman, Avdiivka na Maryinka.

Vikosi vya Urusi vimendelea kuchukua zaidi ya kilomita za mraba 45,000 kusini mwa Ukraine, ukiachilia mbali eneo la Rasi ya Crimea na sehemu za kusini mwa Donetsk zilizochukuliwa mnamo 2014.

Soma pia:Ukraine yasema uwezo wa angani wa Urusi ni tatizo kubwa

Mapema leo Jumatatu, jeshi la anga Ukraine limedungua ndege zisizokuwa na rubani 13 kati ya 17.

Kwa upande mwengine, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky akisema meli za Urusi zimerejea nyuma huko katika Bahari Nyeusi.

"Adui hakika hawezi kuamua hali katika Bahari Nyeusi" Alisema Zelensky katika hotuba yake ya kila siku kupitia mkanda wa video.

Amesema wakaazi watalazimika kuogopa kukaribia Crimea na pwani ya Bahari ya Azov.

"Meli za Urusi tayari zinaogopa kukaribia pwani yetu ya Bahari Nyeusi."

Kostin:Urusi kufadhili Wagner ni ushahidi wa wazi

Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Ukraine Andriy Kostin akiwa mjini The Hague kwenye ufunguzi wa Kituo cha Kimataifa cha Mashtaka ya Uhalifu na Uchokozi leo Jumatatu, amesema ofisi yake imemtambua Yevgeny Prigozhin kama mshukiwa wakati wa uchunguzi mwaka huu.

Akielezea namna kundi hilo lilivyotekeleza uhalifu wa kivita anasema, wapiganaji wa Wagner walihusika na baadhi ya uhalifu mkubwa wa kivita tangu uvamizi wa Februari 2022.

Soma pia:Mkuu wa Wagner asema jeshi la Urusi linamdanganya Rais Putin

Amesema wakati Urusi inajaribu kutofautisha kati ya vikosi vya Wagnerna jeshi lake, maoni ya Rais Vladmir Putin wiki iliyopita kuhusu matumizi ya bajeti ya serikali kwa Wagner yalikuwa ni ushahidi wa moja kwa moja kuwa kikosi hicho haramu kinahusika katika uhalifu:

"Hivyo ni sehemu nyingine ya shughuli zao haramu." alisema Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Ukraine.

Aliongeza kwamba si tu haramu, lakini ni wamefanya uhalifu mbaya zaidi

"Wamefanya uhalifu mbaya dhidi ya raia wetu na wafungwa wa vita."

Wiki iliyopita, Putin alisema kwamba Wagner chini ya uongozi wa Prigozhin, walipokea karibu dola bilioni 2 kutoka Urusi katika mwaka uliopita.

Wataalamu wa masuala ya usalama wanasema kundi la Wagner ni tishio sio tu kwa Ukraine, bali kwa amani na usalama katika nchi nyingi, ikiwa ni pamoja na Amerika ya Kusini, Afrika na Mashariki ya Kati.

Kundi la Wagner lingewezaje kuasi Afrika?