1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uingereza yatoa amri ya Assange kushtakiwa Marekani

20 Aprili 2022

Mahakama ya Uingereza imetoa uamuzi wa kumpeleka Marekani mwanzilishi wa tovuti ya ufichuzi wa taarifa ya WikiLeaks Julian Assange ajibu mashtaka ya uchapishaji wa nyaraka za siri zinazohu vita vya Iraq na Afghanistan

https://p.dw.com/p/4A9tL
Julian Assange
Picha: Peter Nicholls/REUTERS

Kwa sasa uamuzi wa mwisho anao waziri wa mambo ya ndani wa Uingereza Priti Patel, ingawa Assange bado anaweza kukata rufaa ndani ya siku 14. 

Uamuzi huu uliyotolewa na hakimu katikati mwa jiji la London unalielekeza katika hitimisho sakata hili la muda mrefu katika Mahakama za Uingereza. Lakini mawakili wa Assange kufikia Mei 18 wanaweza kuwasilisha hoja zao kwa Patel na hata kukata rufaa zaidi kuhusiana na maswala katika kesi hiyo.

soma zaidi: Julia Assange aruhusiwa kukata rufaa Uingereza

Mawakili wa Assange wamesema hadi sasa hakuna rufaa yeyote iliyowasilishwa kwenye Mahakama Kuu. Kesi hiyo imekuwa mfano wa kuigwa kwa uhuru wa vyombo vya habari, huku wafuasi wa Assange wakiishutumu Washington kwa kujaribu kuzuia masuala muhimu ya kiusalama kuripotiwa.

soma zaidi: Uingereza yakataa kumrejesha Julian Assange Marekani

Nje ya mahakama, waandamanaji walionyesha mabango yaliyoandikwa "Assange asirejeshwe" huku wakipachika kwenye kuta nje ya mahakama, vijitambaa vya njano vya kutaka Assange aachiliwe huru.

Uamuzi wa Uingereza ni sawa kutoweka kwa demokrasia

Großbritannien | Unterstützer fordern die Freilassung von Julian Assange
Wafuasi wa Julian Assange mjini London, wakionyesha mabango yanayoping Assange kupelekwa MarekaniPicha: Alberto Pezzali/AP Photo/picture alliance

Mwandishi wa habari na mwanaharakati wa Assange Carolina Graterol, kutoka Venezuela, ameuita uamuzi huo kuwa ni siku nyingine ya kutoweka demokrasia na utawala wa sheria nchini Uingereza. Graterol ameliambia shirika la habari la AFP kuwa uamuzi uliochukuliwa na jaji wa kurejeshwa Assange, ni ukiukaji wa haki na kwamba anadhani Assange atafia jela kwa huzuni iwapo atarejeshwa Marekani.

Mwezi uliopita, Assange alinyimwa kibali cha kukata rufaa katika Mahakama ya Juu ya Uingereza dhidi ya hatua ya kumrejesha Marekani, ambako anaweza kuhukumiwa kifungo cha maisha jela. Washington inataka kumfungulia mashtaka kuhusiana na uchapishaji wa faili 500,000 za siri na za kijeshi zinazohusiana na vita vinavyoongozwa na Marekani nchini Iraq na Afghanistan.

Mwezi Januari mwaka jana, raia huyo wa Australia mwenye umri wa miaka 50 alionekana kupata ahueni kwa kigezo kuwa alikuwa katika hatari ya kujiua ikiwa angewekwa kizuizini katika jela zenye usalama mkali huko Marekani.

Lakini serikali ya Marekani ilikata rufaa na kutoa hakikisho la kidiplomasia kwamba Assange hatoadhibiwa wala kuwekwa katika kizuizi cha upweke katika gereza kuu na kwamba angelipewa huduma zinazostahili. Assange pia alikata rufaa dhidi ya uamuzi huo.

Hakimu Paul Goldspring amesema kuwa, "anawajibika" kupeleka kesi hiyo kwa waziri wa mambo ya ndani wa Uingireza Priti Patel kulingana na uamuzi wa mahakama ya juu zaidi nchini humo.

Assange anatafutwa kujibu mashtaka kwa kukiuka Sheria ya Ujasusi ya Marekani kwa kuchapisha faili za kijeshi na kidiplomasia mnamo mwaka 2010. Anaweza kukabiliwa na kifungo cha miaka 175 jela iwapo atapatikana na hatia, ingawa vigumu kukadiria hukumu kamili.

Chanzo: AFP