1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiAsia

Shughuli za uokozi zaendelea usiku kucha Uturuki na Syria

Daniel Gakuba
8 Februari 2023

Waokoaji wamefanya kazi usiku kucha nchini Uturuki na Syria kutafuta manusra wa tetemeko la ardhi lililotokea Jumatatu, Lakini hali mbaya ya hewa na baridi kali vinafifisha matumaini ya kuwapata wengi wakiwa bado wazima.

https://p.dw.com/p/4NDFJ
Türkei Hatay Erdbeben Rettungsaktion
Picha: Umit Bektas/REUTERS

 Wafanyakazi wa vitengo vya dharura wa Uturuki na Syria wanaungwa mkono na wengine kutoka duniani kote, huku msaada wa kimataifa ukiendelea kuwasili. Maafisa wanasema idadi ya waliouawa na tetemeko la Jumatatu imefika watu 7,926 katika nchi hizo mbili.

Soma zaidi: Erdogan atangaza hali ya dharura katika maeneo ya tetemeko

Makamu wa Rais wa Uturuki Fuat Oktay alisema jana Jumanne kwamba watu 5,894 wameuawa na 34,810 wamejeruhiwa nchini Uturuki, wakati shughuli za utafutaji zikiendelea takribani saa 48 tangu tetemeko la kwanza kutokea.

Nchini Syria, shirika la habari la serikali SANA liliripoti kuwa watu 812 wameuawa na 1,449 kujeruhiwa katika maeneo yanayodhibitiwa na serikali. Shirika la White Helmet linaloratibu juhudi za uokoaji katika eneo linaloshikiliwa na waasi limesema  watu 1,220 waliuawa na 2,600 kujeruhiwa.

Türkei Osmaniye Erdbeben Trauer
Walionusurika tetemeko hili wamo katika hali ya majonzi makubwa kwa kupoteza kila kituPicha: Khalil Hamra/AP Photo/dpa

Jumuiya ya kimataifa yajitolea kusaidia

Timu za waokoaji kutoka Korea Kusini, Marekani, Bosnia-Herzegovina, Ujerumani, Umoja wa Falme za Kiarabu -hizo zikiwa baadhi tu ya nchi zilizotuma msaada -  zimejiunga na oparesheni za kuwatafuta watu chini ya kifusi, huku matumaini ya kuwapata walio bado hai yakiendelea kufifia.

Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani,  USAID, limesema vikundi viwili vya wataalamu wake wa uokoaji zimewasili Uturuki mapema Jumatano.

Soma zaidi: Nchi duniani kote zinahamasisha misaada ya haraka kwa ajili ya Syria na Uturuki

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ujerumani Nancy Faeser alisema  waokoaji wapatao 40 kutoka shirika la misaada la Ujerumani (ISAR Ujerumani) walikuwa tayari nchini Uturuki, pamoja na maafisa kadhaa wa jeshi la polisi la shirikisho la Ujerumani. Timu nyingine ya wataalamu kutoka shirika la uokoaji la THW ilichelewa kuondoka Jumanne kwa sababu yahali mbaya ya hewa.

Südkorea Incheon | Rettungsteam vor dem Flug ins Erdbebengebiet in der Türkei
Nchi nyingi duniani zimepeleka wataalamu wa uokoaji pamoja namsaada wa kibinadamuPicha: Ahn Young-joon/AP Photo/picture alliance

Waturuki wa Ujerumani wakusanya msaada kwa ajili ya wenzao nyumbani

Huko Berlin, vikundi vya jamii vya Waturuki na Wakurdi viliratibu kukusanya, kupanga, na kutuma michango ya misaada kutoka kwa watu wa jamii hizo wanaoishi Ujerumani. Operesheni kama hizo zilikuwa zikiendelea pia Frankfurt na Munich.

Umoja wa Mataifa umetoa dola milioni 25  kutoka mfuko wake wa dharura kwa ajili ya msaada wa kibinadamu kwa waathiriwa wa tetemeko la ardhi nchini Uturuki na Syria.

Kamishna wa Umoja wa Ulaya anayeshughulikia mizozo Janez Lenarcic amesema timu 27 za waokoaji kutoka nchi 19 wanachama wa Umoja wa Ulaya zimepelekwa Uturuki kusaidia. Amesema timu hizo zinajumuisha  wataalamu 1150 na mbwa 70 wenye mafunzo ya kunusa.

 

Vyanzo: msh/wd (AFP, AP, dpa, Reuters)