1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Pompeo afanya mazungumzo na Netanyahu na Gantz

Saumu Mwasimba
13 Mei 2020

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo na waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu wamejadiliana masuala kadhaa ikiwemo mpango wa Israel wa kutaka kuyatwaa maeneo zaidi ya Ukingo wa Magharibi. 

https://p.dw.com/p/3cAwT
Israel Premierminister Netanjahu und US-Außenminister Pompeo
Picha: picture-alliance/dpa/K. Gideon

Viongozi hao wawili walitowa taarifa kila mmoja kabla ya mkutano wao kuanza mjini Jerusalem leo hii na Netanyahu alimkaribisha Pompeo na kutowa shukurani kwa Marekani kwa kuliunga mkono kwa dhati dola la Israel ,na ushirikiano katika kukabiliana na janga la mripuko wa kirusi cha Corona pamoja pia na kuendelea kwa juhudi za kudhibiti shughuli za Iran katika ukanda huo. Kadhalika Pompeo alisisitiza juu ya kazi iliyobakia ya kuchukua hatua kuhusu mpango wa amani ya mashariki ya kati ulioandaliwa na serikali ya rais Trump.

Pompeo alinukuliwa akisema "Tutapata nafasi ya kuzungumzia mwelekeo wa amani. Mpaka sasa imepita miezi kadhaa tangu ulipokuja Washington wakati rais Trump alipoutangaza mpango wa amani''

Katika ziara yake hii waziri huyo wa mambo ya nje wa Marekani atakutana pia na spika wa bunge la Israel, Knesset Benny Gantz leo kabla ya kurejea Marekani baadae.

Israel | USA | Mike Pompeo |  Benny Gantz
Waziri Pompeo pia alikutana na spika wa bunge la Israel, Knesset na kujadili masuala kadha wa kadhaPicha: Reuters/S. Scheiner

Kwa mujibu wa Netanyahu suala la janga la Corona litazungumziwa kwa kina akisema kwanza kabisa janga hilo ni changamoto ya dunia kwa ujumla,zikiwemo Marekani na Israel.

Lakini pia kubwa linalogusiwa kwenye mkutano huo ni kuhusu kuimarishwa ushirikiano wa nchi hizo mbili , katika mapambano dhidi ya janga hilo. Lakini pia kumbuka ziara hii ya siku moja ya mwanadiplomasia huyo wa Marekani nchini Israel imekuja wakati kukiwa na hali ya mashaka hasa baada ya mwanajeshi mmoja wa Israel kuuwawa na wapalestina na kijana wakipalestina kuuwawa kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa Israel katika ardhi ya wapalestina iliyonyakuliwa kwa mabavu na Israel.Mipango ya Trump kuigeuza Jordan kuwa taifa la Palestina

Wanajeshi wa Israel wameanzisha msako mkali wa kuwatafuta waliomuua mwanajeshi mwenzao wakati jeshi hilo lilipovamia kijiji kimoja huko Ukingo wa Magharibi. Mwanajeshi huyo wa Israel aliuliwa kwa jiwe lililoporomoshwa kutoka kwenye paa la nyumba.

Ingawa mpaka sasa sio Netanyahu wala Pompeo aliyezungumzia au kutaja vurugu zilizotokea leo Kusini mwa Ukingo wa Magharibi kati ya jeshi la Israel na vijana wa kipalestina.

Suala muhimu ambalo pia msikilizaji anapaswa kulifahamu katika mpango wa Israel wa kutaka kuyanyakua maeneo zaidi ya wapalestina Ukingo wa Magharibi ni kwamba rais Donald Trump anakabiliwa na uchaguzi mwezi Novemba na Netanyahu na kambi yake wanapania kuharakisha mpango huo ambao kwa upande wa Trump utampa nguvu ya kuungwa mkono na wapiga kura wakimarekani wanaoipendelea Israel.