1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tundu Lissu na wenzake waachiwa kwa dhamana

Veronica Natalis
11 Septemba 2023

Jeshi la polisi mkoani Arusha limemwachia kwa dhamana makamu mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, Chadema Tundu Lissu na wenzake watatu waliokamatwa jana Jumapili wakiwa wilayani Karatu mkoani humo.

https://p.dw.com/p/4WBuF
Makamu mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, CHADEMA, Tundu Lissu akiwasili nchini Tanzania akitokea Ubelgiji alikokuwa akiishi kwa muda mrefu.
Makamu mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, CHADEMA, Tundu Lissu akiwasili nchini Tanzania akitokea Ubelgiji alikokuwa akiishi kwa muda mrefu.Picha: Eric Boniface

Tundu Lissu na wenzake walikuwa wakijiandaa na ziara ya mkutano wa hadhara katika tarafa ya Loliondo wilaya ya Ngorongoro na polisi wanasema walimkamata kwa sababu hakuwa na kibali cha kufanya mkutano huo wa hadhara. 

Tundu Lissu aliwahutubia maelfu ya wananchi tarafa ya Loliondo mwishoni mwa juma lililopita baada ya kutoka wilaya ya Mugumu, Serengeti mkoani Mara, ikiwa ni mwendelezo wa chama cha Chadema wa kuyafikia maeneo mbalimbali ya Tanzania kwa kufanya mikutano ya hadhara.

Baada ya mkutano huo Lissu na ujumbe wake walianza kuelekea katika tarafa ya Ngorongoro kwa ajili ya mkutano mwingine wa hadhara ndipo walipozuiwa na jeshi la polisi kwa madai kuwa hawakuwa na kibali cha kufanya mkutano huo. Walipelekwa katika kituo cha polisi mkoani Arusha kaskazini mwa Tanzania na wakaachiwa kwa dhamana Jumapili usiku.

Lissu alinukuliwa akisema "Haya ni makosa ya kisiasa. Hawawezi kuzijibu hoja ambazo tumezizungumza kuhusiana na wanachi wa Ngorongoro kuondolewa. wanajaribu kutumia sheria za jinai ili kuficha aibu ya wao kushindwa kujibu hoja zinazohusiana na serikali kujaribu kuwahamisha wananchi wa Ngorongoro.."

Wakazi hawa wakiwa wamendamana kupinga hatua ya serikali ya Tanzania ya kuwaondoa kwenye eneo lao huko Ngorongoro
Tundu Lissu anasema serikali inachukua hatua ili kuficha aibu yao kufuatia hatua za kuwaondoa wakazi wa Ngorongoro.Picha: Deinis Olushangai

Taarifa ya maandishi ya jeshi la polisi mkoani Arusha iliyotolewa na kamanda wake Justine Maseje inaeleza kwamba inamshilikilia Lissu pamoja na wenzake watatu kwa mahojiano kwa tuhuma za kufanya mikusanyiko isivyo halali pamoja na kuwazuia askari polisi kutekeleza majukumu yao na kwamba baada ya mahojiano, taratibu nyingine za kipolisi zitafuata.

Katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa X mwenyekiti wa taifa wa Chadema Freeman Mbowe, alilaani kukamatwa kwa Lissu na wenzake, akisema kwa sasa chama chake kina hofu na usalama wa viongozi na wanachama wake.

Tuhuma zinazomkabili Tundu Lissu na wenzake zipo chini ya kifungu cha sheria cha 74 cha sheria ya jinai ya Tanzania ambapo pamoja na mambo mengine, kizuia mikusanyiko isiyokuwa na kibali cha polisi. Lissu na wenzake walitakiwa kuripoti leo polisi kwa ajili ya mahojiano zaidi.

Hili ni juma la tatu la ziara ya CHADEMA katika maeneo mbalimbali ya Tanzania, ambapo chama hicho kimejipanga kuwafikia wananchi kwa kufanya mikutano ya hadhara.