1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nchi za Ulaya kutoa cheti cha Covid-19 kwa raia wake

21 Mei 2021

Bunge la Ulaya na nchi wanachama wa Umoja wa Ulaya wamefikia makubaliano ya kutoa cheti cha Covid-19 ambacho kitatoa nafasi ya usafiri kote barani Ulaya katika kipindi cha utalii cha majira ya joto.

https://p.dw.com/p/3tiT8
Symbolbild | Brexit | Millionen EU-Bürger wollen in Großbritannien bleiben
Picha: Nicolas Economou/NurPhoto/picture alliance

Haya yanakuja wakati ambapo utafiti uliochapishwa hii Ijumaa umeonyesha kwamba wagonjwa mahututi wa Covid-19 barani Afrika wako katika hatari kubwa ya kufariki dunia ikilinganishwa na katika mabara mengine duniani.

Kamishena wa masuala ya haki wa Umoja wa Ulaya Didier Reynders baada ya majadiliano kuhusiana na cheti hicho na wabunge wa Umoja huo na Ureno ambayo ndiyo nchi inayoshikilia urais wa kupokezana wa Umoja wa Ulaya, aliandika kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter akisema, "hatimaye tuna moshi mweupe."

Cheti kitazuia hasara ya kutokuwepo na utalii Ulaya

Makubaliano hayo yatatoa nafasi kwa mtu yeyote anayeishi katika nchi ishirini na saba za Umoja wa Ulaya kupata pasi ya kidijitali kufikia mwishoni mwa mwezi Juni itakayokuwa inaonyesha hali yake ya chanjo, majibu yake ya vipimo vya Covid-19 au iwapo wamepona maambukizi ya virusi vya corona.

Argentinien Corona-Pandemie | Impfkampagne
Mhudumu akichoma chanjo ya Covid-19Picha: Natacha Pisarenko/AP Photo/picture alliance

Cheti hiki kinasemekana kitazuia hasara ambayo huenda ingepatikana katika kipindi cha majira ya joto Ulaya ambapo watu wengi husafiri katika nchi tofauti kwa ajili ya utalii. Juan Fernando Lopez ni mmoja wa maafisa wa Umoja wa Ulaya waliohusika katika majadiliano hayo.

"Hii ni kwa ajili ya kuweza kuaminiana tena, sio tu kwa wanachama wa Umoja wa Ulaya lakini pia raia wa Ulaya ili kimsingi waweze kufurahia haki yao ya kusafiri bila vizuizi," alisema Lopez.

Kwengineko utafiti uliofanywa na hospitali ya Groote Schuur na Chuo Kikuu cha Capetown nchini Afrika Kusini unaonyesha kuwa wagonjwa wa virusi vya corona barani Afrika wako katika hatari kubwa ya kufariki kwasababu ya ukosefu wa vifaa muhimu vya matibabu.

Amerika Kusini inatarajiwa kupokea mamilioni ya chanjo

Utafiti huo ulifanyiwa wagonjwa elfu tatu wa Covid-19 waliokuwa wamelazwa katika vyumba vya wagonjwa mahututi katika nchi kumi za Afrika kati ya mwezi Mei na Desemba mwaka jana na ukapata kuwa nusu ya wagonjwa hao walifariki ndani ya siku 30 walizolazwa hospitali.

Impfstoff Pfizer-BioNTech COVID-19
Chanjo ya Pfizer-BioNTechPicha: Christof STACHE/AFP

Huku hayo yakiarifiwa nchi za Amerika Kusini zinatarajiwa kupokea mamilioni ya chanjo zilizotrengenezwa Marekani katika kipindi cha wiki chache zijazo. Argentina inatarajiwa kuongeza muda wa vikwazo vya kutotoka nje kufuatia ongezeko la maambukizi wiki iliyopita.

Huko Asia nako Japan inatarajiwa kuongeza hali ya dharuira katika kisiwa cha kusini cha Okinawa hii leo wakati ambapo nchi hiyo imeidhinisha chanjo mbili za virusi vya corona ili kuharakisha kampeni yake ya utoaji chanjo.