1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Muswada wa vyama vya siasa kuhanikiza Bunge la Tanzania

Iddi Ssessanga29 Januari 2019

Bunge la Tanzania limefanya kikao chake cha kwanza cha mkutano wa 14 mjini Dodoma huku mambo mbalimbali yakijadiliwa ikiwemo kusomwa kwa mara ya pili mswada wa marekebisho ya sheria ya vyama vya siasa wa mwaka 2018.

https://p.dw.com/p/3CO2P
Tansania Parlament Dodoma - Parlamentsvorsitzende mit Philip Mpango und Premierminister Kassim Majaliwa
Picha: DW/S. Khamis

Hata hivyo upinzani umeendelea kuonesha mashaka juu ya baadhi nya vifungu vilivyomo katika mswada huo na kudai una lengo la kuviminya vyama vya siasa kufanya kazi zake kwa uhuru na demokrasia. 

Mara baada ya kuwasilishwa kwa mswada huo bungeni hii leo na kisha kusomwa kwa mara ya pili na Waziri wa nchi, ofisi ya Waziri mkuu-(Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na watu wenye ulemavu) Jenista Muhagama, ilifuata hotuba ya msemaji mkuu wa kambi ya upinzani bungeni na kisha kufuatia michango kutoka kwa wabunge mbalimbali kuhusiana na Mswada huo.

Akiwasilisha maoni ya kambi rasmi ya upinzani katika ofisi ya waziri mkuu kuhusiana na mswada huo wa marekebisho ya sheria ya vyama vya siasa wa mwaka 2018, msemaji mkuu wa kambi rasmi ya upinzani bungeni Ester Bulaya amesema kuwa kuna baadhi ya vifungu ndani ya mswada huo vimelenga kuvibana vyama vya siasa na hivyo kuhatarisha uhai wa vyama hivyo katika siku za usoni.

Kwa upande wao wabunge wa CCM wamesema kuwa Mswada huo umekuja wakati mwafaka na kwamba utajenga taifa lenye nidhamu, demokrasia, amani na utulivu na kwamba viongozi wa vyama vya siasa waliokuwa wakiendesha vyama kama mali zao binafsi ni mwarobaini kwao, kama anavyoelezea Joseph Muhagama mbunge kupitia CCM.

Lakini mbunge wa Kawe kupitia tiketi ya CHADEMA Halima Mdee, amesema kuwa CCM ambayo imepewa dhamana ya kuongoza Tanzania inapaswa kusema ukweli katika hili na iache kuwadanganya wananchi kuwa yenyewe ina uchungu na watu wanaokuwa wakitumia vibaya fedha za umma.

Kikao cha pili cha mkutano huo wa 14 cha bunge la jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kitaendelea tena hapo.

Mwandishi:  Deo Kaji Makomba, DW Dodoma.

Mhariri: Iddi Ssessanga