1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makamu wa rais zimbabwe yuko Afrika Kusini kwa matibabu

Grace Kabogo
4 Februari 2019

Constantino Chiwenga ambaye ni makamu wa rais Zimbabwe, yuko Afrika Kusini kutibiwa. Gazeti binafsi la Zimbabwe limeripoti kuwa afya ya Chiwenga, mwenye umri wa miaka 62 inafuatiliwa kwa ukaribu zaidi na Zimbabwe

https://p.dw.com/p/3Cfxl
Zimbabwe Vizepräsident Constatino Chiwenga
Picha: Reuters/P. Bulawayo

Makamu wa Rais wa Zimbabwe, Constantino Chiwenga anatibiwa nchini Afrika Kusini, ikiwa ni kwa mara ya pili katika kipindi cha miezi minne, baada ya kuugua wiki iliyopita.

Gazeti binafsi la Zimbabwe limeripoti leo kuwa afya ya Chiwenga, mwenye umri wa miaka 62 inafuatiliwa kwa ukaribu zaidi na Zimbabwe, kwa sababu anaonekana kama ni mtu mwenye mamlaka nyuma ya Rais Emmerson Mnangagwa na anayeonekana kumrithi kiongozi huyo.

Gazeti la News Day limesema wiki iliyopita Chiwenga aliwasili katika hospitali binafsi, lakini ilimbidi asafiri hadi Cape Town, Afrika Kusini kwa matibabu zaidi. Msemaji wa ofisi ya rais, George Charamba amesema leo kuwa hawezi kutoa ufafanuzi kuhusu suala hilo.

Mwezi Oktoba, mwaka uliopita Charamba alisema kuwa Chiwenga alisafiri kwenda Afrika Kusini kwa matibabu baada ya kujeruhiwa kutokana shambulizi la bomu lililotokea wakati wa mkutano wa kampeni wa Mnangagwa kabla ya uchaguzi wa Julai 30.