1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yawaokoa mateka wanne kutoka kambi ya wakimbizi Gaza

9 Juni 2024

Israel imetangaza imewaokoa mateka wanne kutoka kambi moja ya wakimbizi huko Gaza katika operesheni ambayo ofisi ya habari ya serikali inayoongozwa na Hamas inasema ilisababisha vifo vya Wapalestina 210.

https://p.dw.com/p/4gpiJ
Mateka wa Israel waokolewa Gaza
Jamaa na familia za mateka walioachiwa walifika kukutana na wapendwa wao katika hospitali ya Tel HashomerPicha: Ilia Yefimovich/dpa/picture alliance

Jeshi la Israel limesema mateka hao wanne,ambao walikuwa katika hali nzuri ya kiafya, walitekwa nyara kutoka kwenye tamasha la muziki la Nova wakati wa shambulizi la Hamas la Oktoba 7.

Shambulizi hilo lilichochea vita, ambavyo sasa vipo katika mwezi wake wa tisa. Mateka hao ni miongoni mwa saba ambao vikosi vya Israel vimewaokoa wakiwa hai tangu wanamgambo wa Kipalestina walipowakamata watu 251 katika shambulizi lao la Oktoba kusini mwa Israel. Jeshi limesema sasa kuna mateka 116 waliobaki Gaza, wakiwemo 41 ambao jeshi linasema wameuawa.

Soma pia: Israel yaendeleza mashambulizi Gaza wakati waziri wa vita akitishia kujiuzulu

Wakati huo huo, msaada umeanza kuingizwa tena Ukanda wa Gaza hapo jana kwa kutumia gati ya muda iliyojengwa upya. Hayo ni kwa mujibu wa Kamandi kuu ya Marekani CENTCOM. CENTCOM imesema ilipeleka tani 492 za msaada unaohitajika kwa dharura kwa kutumia gati hiyo jana asubuhi na kusisitiza kuwa kituo hicho hakihusiani kwa vyovyote vile na operesheni ya Israel kuwaokoa mateka.