Wanamgambo wa Palestina wafyatua makombora dhidi ya Israel
21 Septemba 2025
Jeshi la Israel limesema kwamba wanamgambo wa Kipalestina katika Ukanda wa Gaza wamefyatua makombora mawili kuelekea Israel mapema leo Jumapili. Katika taarifa yake, jeshi la Israel IDF, limeongeza kuwa kombora moja limedunguliwa na mfumo wake wa ulinzi wa anga na jingine limeanguka katika eneo la wazi. Ving'ora vya tahadhari vimesikika katika mji wa bandari wa Ashdod, kaskazini mwa Ukanda wa Gaza na katika eneo la Lachish, kusini magharibi mwa Jerusalem. Bado haijafahamika ni kundi gani la wanamgambo lililohusika na shambulio hilo. Israel imeshambuliwa kwa maelfu ya makombora yanayorushwa kutoka eneo la pwani tangu kuanza kwa vita vya Gaza mwezi Oktoba mwaka 2023, lakini mashambulizi hayo yamepungua katika siku za hivi karibuni. Israel imeendesha vita dhidi ya kundi la Hamas kwa takriban miaka miwili sasa.