1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ghasia dhidi ya wanawake wanaowania viti vya siasa Kenya

John Juma
1 Agosti 2022

Kenya inapojiandaa kwa uchaguzi mkuu Agosti 9, baadhi ya wanawake wanaowania viti vya kisiasa wanakumbwa na matukio ya ghasia dhidi yao kipindi wanaposhiriki siasa.

https://p.dw.com/p/4ExBE
BdTD | Kenia
Picha: Luis Tato/AFP

Liz Njue, mwanamke mwanasaikolojia nchini Kenya aliyetaka kuwania kiti cha ubunge katika kaunti, alivamiwa na wapinzani punde tu alipowasili katika kituo cha kupiga kura wakati wa uteuzi wa wagombea wa vyama vya siasa. Ilimbidi achane mbuga bila hata kupiga kura na hivyo ndivyo alivyopeteza nafasi hiyo.

Kulingana na chama cha wabunge wanawake nchini Kenya, Njue ni kati ya makumi ya wanawake wanaowania nyadhifa mbalimbali za kisiasa ambao wamevamiwa wakati wa kampeni kuelekea uchaguzi wa Agosti 9.

Ghasia kama hizo huwazuia wanawake wengi kushiriki siasa ila wachache walio ngangari. Kulingana na Mercy Mwangi ambaye ni mratibu wa chama hicho, visa vingi kama hivyo hukosa kuangaziwa.

"Watu wanasema tunawataka wanawake kwenye siasa, tunataka wanawake wengi zaidi kuwania viti vya siasa; lakini ni vipi tutawashawishi kuingia katimka siasa ikiwa tutaendelea kuwadhalilisha,” ameuliza Njue aliye na umri wa miaka 39.

Martha Karua, mgombe mwenza wa Raila Odinga (wa muungano wa Azimio) kuwania urais nchini Kenya.
Martha Karua, mgombe mwenza wa Raila Odinga (wa muungano wa Azimio) kuwania urais nchini Kenya.Picha: Thomas Mukoya/REUTERS

Aliripoti tukio dhidi yake kwa polisi, lakini anasema hadi sasa hakuna yeyote aliyekamatwa. Msemaji wa polisi Brunio Isohi Shioho alisema kesi hiyo ingali inashughulikiwa.

Haijulikani wazi ni kina nani hupanga ghasia hizo, lakini wawaniaji wanashuku ni wapinzani wao. Vyama vikuu vya kisiasa havikutoa kauli swali hilo lilipoelekezwa kwao. 

Ghasia dhidi ya wanawake havitokei tu katika nyanja za kisiasa. Takriban nusu ya wanawake nchini Kenya hukabiliwa na dhuluma za kijinsia. Hayo ni kulingana na na kituo kinachoshughulikia manyanyaso ya kijinsia kilichoko hospitali ya wanawake ya Nairobi. 

Mary Mugure, ambaye zamani alikuwa akifanya kazi ya ukahaba alipokea simu pamoja na ujumbe wa vitisho alipokuwa akiwania kiti cha ubunge wa kaunti mwaka huu. Mnamo Novemba, wanaume wawili waliokuwa kwenye pikipiki walimshambulia barabarani.

Mary Mugure anasema hiyo ilikuwa njia moja ya kumtisha ili aachane na kinyang'anyiro hicho. 

Sheria kuhusu idadi ya wawakilishi kwa msingi wa jinsia

Je, IEBC iko tayari kwa uchaguzi wa Kenya?

Ripoti ya utafiti iliochapishwa mwaka 2020 na chuo kikuu cha Cambrige Press, ilisema kipengee cha katiba ambayo imekuwepo kwa zaidi ya muongo mmoja sasa nchini Kenya, kiliweka wazi kwamba jinsia moja isitwae zaidi ya theluthi mbili ya viti vya kisiasa au kwa kuteuliwa- na kwamba labda kipengee hicho kimekuwa sababu ya uvamizi dhidi yao.

Kipengee hicho cha katiba hakijatimizwa itakikanavyo. Wapo wanawake 75 pekee ambao ni wabunge kati ya jumla ya wabunge 349, wakiwemo wanawake 47 ambao ni wawakilishi maalum wa kina mama bungeni. Katika baraza la seneti kuna takriban theluthi moja ya wanawake. Miongoni mwa magavana 47, wapo wanawake watatu pekee.

Matiangi: Tumejiandaa kuilinda Kenya wakati wa uchaguzi

Hakuna mwanamke ambaye amewahi kuwa rais au naibu rais nchini Kenya. Hata hivyo katika uchaguzi wa mwaka huu wagombea wenza wa wawaniaji wawili wa urais Raila Odinga na Wajackoya ni wanawake.Katika nchi jirani, Ethiopia, Tanzania na Uganda, zaidi ya theluthi moja ya wabunge ni wanawake, kulingana na Umoja wa mabunge. Aidha nchini Tanzania na Ethiopia, marais ni wanawake.Kampeni za uchaguzi Kenya zashika kasi

Hata hivyo wakati mwingine kuna matokeo mazuri hata baada ya ghasia. Sarah Korere ambaye ni mbunge wa Laikipia Kaskazini alivamiwa na mshindani wake mwaka 2016.

Lakini alifanikiwa kumbwaga katika uchaguzi uliofuata

(RTRE)