1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
BiasharaAfrika

China na Marekani zalaumiwa kuchelewesha msamaha wa madeni

1 Desemba 2023

Mipango ya msamaha wa madeni inakwenda taratibu, na kuyatesa mataifa yanayoendelea. China imelaumiwa kwa ucheleweshaji wa majibu ya kimataifa. Beijing inapinga na kuitupia lawama Markeani na wakopeshaji inaowaunga mkono.

https://p.dw.com/p/4ZhA7
Ujerumani| Maandamano ya G7
Mataifa mengi yanalazimika kuchagua kati ya kulipa riba au kuwahumia watu wake.Picha: Christian Mang/REUTERS

Yakiwa yamekumbwa na majanga mengi kama vilejanga la COVID-19, vita nchini Ukraine na mabadiliko ya tabianchi, mataifa yanayoendelea, mengi yakiwa barani Afrika, yalirundika viwango vya juu vya madeni ili kudumisha uchumi wao. Leo, watu bilioni 3.3 wanaishi katika nchi zinazotumia zaidi kulipa riba ya madani kuliko elimu au afya, kulingana na Umoja wa Mataifa.

Nchi nyingi zinazoendelea zinajikuta katika mazingira magumu katika ulimwengu unaokumbwa na mshtuko, huku hazina zao za kifedha zikipungua katikati mwa ongezeko la gaharama za chakula na nishati; kupanda kwa viwango vya riba nchini Marekani na kwingineko kukiongeza gharama za kukopa kwa serikali; kuongezeka kwa thamani ya dola ya Marekani kunakoongeza riba kwenye mikopo inayotolewa kwa dola; na China, mkopeshaji wao wa kwendea kwa muongo mmoja uliopita, ikishuhudia mdororo mkubwa.

Katika miaka michache iliyopita, takriban nchi 10, zikiwemo Zambia na Sri Lanka, tayari zimekosa kulipa madeni yake, huku zaidi ya nyingine 50 kama vile Pakistan na Misri zikikabiliwa na matatizo ya ulipaji.

Soma pia: G20: Nchi maskini duniani kupata afueni ya madeni?

"Kwa idadi kubwa ya nchi zinazoendelea, mzozo wa madeni unamaanisha pesa ambazo hazijatumika kuleta mabadiliko, uwekezaji wa kubadilisha maisha katika ustawi na maendeleo ya watu, ambao ni 'utajiri wa kweli wa mataifa,'" Achim Steiner, msimamizi wa Mpango wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa, aliiambia DW.

Unafuu wowote kutoka kwa wakopeshaji unachelewa sana kufika huku Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Benki ya Dunia na Klabu ya wakopeshaji ya Paris zikikabiliana na ongezeko la wakopeshaji rasmi wapya kama vile China, India na nchi za Ghuba.

Sri Lanka | Bandari mjini Colombo
Sri Lanka ilikumbwa na mzigo wa madeni hasa kutoka China, yaliopelekea kuporomoka kwa uchumi wake.Picha: Tharaka Basnayaka/NurPhoto/picture alliance

Mgogoro mkubwa wa madeni unaozikabili nchi zinazoendelea ni miongoni mwa mada kuu katika mikutano ya kila mwaka ya IMF na Benki ya Dunia huko Marrakech huku viongozi wakitafuta njia za kuharakisha msamaha wa madeni.

"Ni wakati wa kufadhaisha sana kwa sababu, kwa mtazamo wa kiufundi na kisera, njia iko wazi juu ya jinsi ya kuzipa nchi hizi unafuu huo. Lakini kwa kweli kuna aina ya tatizo kubwa zaidi la kisiasa la kijiografia ambalo linafanya unafuu huo kuwa mgumu sana," Clemence Landers, mwandamizi wa sera katika Kituo cha Maendeleo ya Dunia, aliiambia DW.

Soma pia: Mali yashindwa kulipa madeni yake

Mgogoro wa madeni unaweza pia kuwa na athari kubwa kwa nchi tajiri kwani unawalazimisha watu wengi zaidi kutoka nchi zenye mzigo wa madeni kutafuta hifadhi nje ya nchi. Athari pia inaweza kuonekana katika suala la kupotea kwa mauzo ya nje kwa nchi zenye shida.

Kuibuka kwa China kunatatiza juhudi za masamaha wa madeni

Juhudi za msamha wa madeni zimekuwa zikiongozwa na nchi tajiri wanachama Klabu ya Paris. Hata hivyo, kuuibuka kwa China kama mkopeshaji mkubwa zaidi wa nchi kwa nchi kwa mataifa maskini kumefanya juhudi hizo kuwa ngumu.

China imetoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya dola trilioni moja kwa miradi mikubwa ya miundombinu kama sehemu ya Mpango wake wa Ukanda na Barabara, kwa viwango vya juu vya riba na mara nyingi kwa masharti yasiyoeleweka. Mingi ya mikopo hiyo imekuwa mzigo. Huko nyuma mwaka 2010, ni asilimia 5 tu ya ukopeshaji wa nje wa China ilisaidia wakopaji katika matatizo ya kifedha. Leo, idadi hiyo inafikia asilimia 60, Brad Parks, kutoka AidData, amabyo ni maabara ya utafiti katika chuo kikuu cha William & Mary huko Virginia, aliiambia DW.

Soma pia: IMF, Benki ya Dunia zafanya mikutano ya kwanza Afrika katika kipindi cha miaka 50

Kwa kiasi fulani kwa sababu ya matatizo ya mikopo ya ndani, Beijing imekuwa haiko tayari kupata hasara kwenye mikopo yake, na hapo awali iliepuka juhudi za kimataifa za msamaha wa madeni. Badala yake, ililenga kushughulikia tatizo hilo kwa pande mbili kwa kutoa mikopo ya dharura ya uokoaji au kusimamisha kwa muda marejesho, ikidhania kwamba wakopaji wake walikuwa wakikabiliwa na changamoto za muda mfupi za ukwasi.

Morokko Marrakech IMF Benki ya Dunia
Mkutwano wa IMF na Benki ya Dunia ulifanyika mjini Marrakeshi Oktoba 12, 2023.Picha: Christophe Gateau/dpa

"Beijing sasa inaelewa kuwa baadhi ya wakopaji wake wa mradi wa Ukanda na Barabara wamekwedna mufilisi na unafuu wa ukwasi wa muda mfupi pekee hauwezi kutatua tatizo," Parks alisema.

"Ukifanya kivyako na kuinusuru serikali yenye matatizo ya kifedha bila kuhitaji mageuzi ya sera ya uchumi au uratibu wa kupanga upya deni na wakopeshaji wakuu wote," Parks alisema, "basi unatenegeneza tatizo na kuwaacha wengine kulishughulikia."

Usiri kuhusu mikopo ya China ni suala jingine linalozuia maendeleo ya msamaha wa madeni. Wakopeshaji wasio Wachina, pamoja na wamiliki wa dhamana za kibinafsi, wanasitasita kushiriki katika mazungumzo ya msamaha wa madeni isipokuwa mpaka wafichue sheria na masharti yote yanayokuja na mikopo ya China, wakihofia kwamba wakopeshaji wa China wanaweza kupata upendeleo.

"Ikiwa China itasisitiza kushughulikiwa kama mkopeshaji mkuu ambaye deni lake linahitaji kupewa kipaumbele cha kwanza na wakopeshaji wengine wasukumwe nyuma ya njia ya ulipaji, basi tunaweza kuona miaka na miaka ya mkwamo," Parks alisema.

Taasisi zinazoungwa mkono na Marekani zinapaswa pia kuchukua hasara ya madeni

China imekanusha madai kwamba inakwamisha juhudi za masamaha wa madeni. Gazeti la Global Times linaloungwa mkono na serikali ya nchi hiyo lilisema: "Tuhuma kama hizo zenye nia mbaya ni upuuzi mtupu" - na kuongeza kuwa malipo ya jumla ya malipo ya deni yaliyositishwa na China ndiyo makubwa zaidi miongoni mwa wanachama wa G20.

Soma pia: Benki ya Dunia yazindua mpango wa kusitisha kwa muda malipo ya madeni kwa nchi zilizokumbwa na maafa

Beijing inahoji kwamba, ikiwa itakubali punguzo kwenye mikopo yake, basi hata taasisi za kimataifa kama vile IMF na Benki ya Dunia zinapaswa pia kufuta sehemu ya mikopo yao. Marekani ndiye mbia mkubwa katika wakopeshaji wote wawili.

IMF na Benki ya Dunia hazijapata hasara kwenye madeni yao, zikisema kuwa kufanya hivyo kungedhuru hadhi yao ya wakopeshaji wanaopendelewa, ambayo inawawezesha kutoa mikopo kwa nchi zenye matatizo kwa viwango vya masharti nafuu.

Marekani I Maandamano  IMF Uganda
Waganda walidai kwamba wakopeshaji wanaodhibitiwa na mataifa ya Magharibi washiriki kwenye msamaha wa madeni.Picha: Allison Bailey/NurPhoto/IMAGO

"Ni jambo jipya sana kwa China kuwa mkopeshaji mkuu rasmi. Hili ni jukumu jipya ambalo China inatekeleza duniani," Landers alisema. "Utata hapa ni jinsi ya kuifanya China kuzoea na kufahamu mfumo wa kimataifa ambao dunia nzima inakubaliana nao."

Landers anapendekeza kuunda kundi kama Paris Club la wakopeshaji rasmi wakiwa na China kama mtoa maamuzi mkuu.

"Ni jambo lisilo la kawaida kwamba Klabu ya Paris ndiyo chombo ambacho kinaweka viwango vya marekebisho na kwamba mmoja wa wakopeshaji wakubwa wa nchi kwa nchi kwa mataifa yenye kipato ya chini sio sehemu ya shirika hili," Landers alisema.

Kuibuka kwa wamiliki wa dhamana za kibinafsi

Zikichochewa na ugumu wa kuingia soko la madeni la kimataifa, nchi za Afrika zilitoa hati fungani zenye thamani ya mabilioni kwa wawekezaji wa kimataifa wanaotaka kuweka dau barani Afrika ili wapate faida nyingi. Kuanzia mwaka 2007 hadi 2020, nchi 21 za Afrika ziliuza hati fungani za fedha za kigeni, nyingi kwa mara ya kwanza, kulingana na IMF. Hisa za dhamana za fedha za kigeni za Kiafrika zilifikia dola bilioni 140 (sawa na euro 132 bilioni) mnamo 2021.

Soma pia: Kwanini Marekani iliingia katika mkwamo wa madeni?

Kuibuka kwa wamiliki wa dhamana za kibinafsi kumeongeza ugumu wa juhudi za msamaha wa deni kwani sasa wakopaji inabidi pia kuunda mpango wa usaidizi nao. Mnamo Juni, Zambia, nchi ya kwanza ya Kiafrika kutolipa mkopo wakati wa janga hilo mnamo 2020, ilifikia makubaliano ya kurekebisha deni la dola bilioni 6.3 inazodaiwa na wakopeshaji rasmi, pamoja na China, lakini haijaweza kufanya makubaliano na wamiliki wake.

Kundi la nchi za G20 limeunda mfumo mpya wa pamoja wa kurekebisha madeni, kuwaleta pamoja wanachama wa Klabu ya Paris na wakopeshaji wengine. Mbinu hiyo ya umoja imepata maendeleo fulani katika miezi ya hivi karibuni.

IMF inasema ilichukua Chad miezi 11 mwaka 2021 kupata ahadi kutoka kwa wakopeshaji wake kutoa msamaha wa deni unaohitajika. Kwa upande wa Zambia, ilichukua miezi tisa, miezi sita kwa Sri Lanka na miezi mitano kwa Ghana.

"Bado ni juu ya miezi miwili au mitatu ambayo tuliona huko nyuma. Kwa hivyo bado sio mahali ambapo tungependa kuwa, lakini ni maendeleo makubwa," Guillaume Chabert, naibu mkurugenzi wa Idara ya Mikakati na Ukaguzi wa Sera ya IMF, aliiambia DW.