1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Buhari apata ushindi wa kwanza Nigeria

Iddi Ssessanga
25 Februari 2019

Waangalizi wa uchaguzi wanakosoa kuchelewesha ufunguaji wa vituo katika maeneo mengi nchini Nigeria, wakisema uchelewashaji huo na kuahirishwa kwa uchaguzi huo kwa wiki nzima viliwakatisha tamaa watu wengi kupiga kura.

https://p.dw.com/p/3E4Pq
Nigerias Präsident Buhari und sein Vize beim APC-Parteitag
Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari na makamu wake Yemi Osibanjo.Picha: Novo Isioro

Ujumbe wa waangalizi wa Umoja wa Afrika umesema katika ripoti yake kuwa uchaguzi ulipita kwa amani kwa sehemu kubwa licha ya matukio kadhaa wa kadhaa ya vurugu na udanganyifu.

Kundi la Situation Room, ambalo ni muungano wa mashirika ya kiraia yaliosimamia uchaguzi huo kw apamoja, limesema watu wasiopungua 39 waliuawa nchini Nigeria kote kwenye siku ya uchaguzi.

Kundi la waangalizi wa Jumuiya ya Madola limezitaja vurugu zilizoukumba uchaguzi huo kuwa suala linalohuzunisha na mwenyekit wake, rais wa zamani wa Tanzania Jakaya Kikwete amesema Nigeria ingeweza kufanya vizuri zaidi.

"Kumekuwa na ugumu wa kimandalizi, kilojistiki na kiufundi katika uchaguzi huu ambavyo tunajua na kuamini kuwa INEC na wadau wote nchini Nigeria watahitaji kuvishughulikia.

Jambo la pili, vurugu zinazohusiana na uchaguzi na upotevu wa maisha vilivyotokea katika maeneo kadhaa vinasikitisha. Naamini Nigeria inaweza kufanya vizuri zaidi. Vurugu hazina nafasi katika demokrasia ya kisasa."

Mkuu wa ujumbe wa waangalizi wa Umoja wa Ulaya Maria Arena amesema kura hiyo ilitatizwa na kosoro za kiutendaji zilizosababisha ugumu kwa wapigakura.

Vor Wahlen in Nigeria  Muhamadu Buhari (M), Präsident von Nigeria, und Atiku Abubakar (r)
Mshindani mkuu wa Buhari, Atiku AbubakarPicha: picture-alliance/AP/B. Curtis

Nalo kundi la waangalizi kutoka Marekani limesema ucheleweshaji wa uchaguzi huo kwa wiki nzima umeharibu imani ya umma katika mchakatohuo na yumkini kupunguza uitikiaji wa wapigakura.

Kinyangang'anyiro kikali zaidi

Haijabainika wazi lini mshindi atatangazwa lakini kura hiyo inayompambanisha rais wa sasa Muhammadu Buhari dhidi ya mfanyabiashara na makamu wa zamani wa rais Atiku Abubakar inatazamiwa kuwa kinyang'anyiro kikali zaidi nchini Nigeria tangu kumalizika kwa utawala wa kijeshi mwaka 1999.

Matokeo ya mwanzo yaliotolewa na tume huru ya uchaguzi INEC, kutoka majimbo mawili kati ya 36, yote ya kusini magharibi mwa nchi, yamemuweka mbele Buhari kwa asilimia 58 dhidi ya 40 katika jimbo la Ekiti, na 49 dhidi ya 47 katika jimbo la Osun.

Ushindi wa kwanza wa Abubakar ulikuwa katika mji mkuu wa shirikisho Abuja, ambako alimshinda Buhari kwa tofauti ya karibu kura 108,000. Buhari pia alishindwa katika kituo cha kura kilichowekwa katika kasri la rais.

Buhari mwenye umri wa miaka 76 na mtawala wa zamani wa kijeshi, anawania muhula wa pili kwa ahadi y akupambana na rushwa, huku Atiku, mwenye umri wa miaka 72, ameahidi juu ya yote, kupanua jukumu la sekta binafsi.

Matokeo yanaonekana kutegemea zaidi yupi kati yao anaaminiwa na wapigakura kufufua uchumi wa taifa hilo unaoendelea kupambana na athari za mdororo wa mwaka 2016.

Mwandishi: Iddi Ssessanga

Mhariri: Mohammed Khelef