1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wengi wajeruhiwa katika maandamano ya Gaza

Bruce Amani
30 Machi 2019

Maelfu ya wakaazi wa Gaza wameandamana katika mpaka wa Israel kuadhimisha mwaka mmoja tangu kuzuka maandamano na machafuko katika Ukanda huo.

https://p.dw.com/p/3FwSY
Gaza | Plästinenser protestieren im Gaza-Streifen
Picha: Getty Images/AFP/M. Hams

Mpalestina mmoja ameuawa na waandamanaji 13 wakajeruhiwa kwa risasi za moto, kwa mujibu wa maafisa wa matibabu wa Kipalestina.

Kundi la Hamas ambalo ndilo linalotawala Ukanda wa Gaza liliahidi kuwaweka waandamanaji mbali na uzio wakati wajumbe wa Misri wakijaribu kufanikisha makubaliano ya kusitisha mapigano.

Lakini baadhi ya waandamanaji waliukaribia ukuta huo, na kupeperusha bendera za Kipalestina na kurusha mawe na miripuko kuelekea upande wa wanajeshi wa Israeli waliokuwa wameweka ulinzi. Wanajeshi wa Israel walijibu kwa kufyatua mabomu ya kutoa machozi ili kuwatawanya waandamanaji hao.

Israel Palästina Gaza Konflikt Protest
Jeshi la Israel lilitumia mizinga ya maji kuwatawanya waandamanajiPicha: Reuters/M. Torokman

Wizara ya Afya ya Gaza ilisema mwandamanaji mwenye umri wa miaka 17 alifariki dunia mara tu baada ya kupigwa risasi usoni mashariki mwa Mji wa Gaza.

Maandamano ya leo yamekuja katika wakati nyeti kwa Israel na Hamas. Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu anatafuta muhula wake wa nne mfululizo madarakani katika uchaguzi wa Aprili 9, lakini anakabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa kundi la wakuu wa zamani wa jeshi ambao wanaikosoa kile wanachosema ni kushindwa kwa sera yake ya Gaza.

Katika hatua za mwisho mwisho za kampeni yake, Netanyahu anahitaji kuleta utulivu katika mpaka wa Israel na Gaza, bila kuonekana kusalimu amri kwa kundi la Hamas. Netanyahu alikosolewa vikali wiki hii kwa kile kilichoonekana kuwa ni msimamo dhaifu dhidi ya mashambulizi mapya ya maroketi kutokea Gaza.

Hamas kwa upande wao, wanakabiliwa na ongezeko la vurugu katika Ukanda wa Gaza kutokana na kuzorota mazingira baada ya Zaidi ya muongo mmoja wa kufungwa kwa mpaka wa Israel na Palestina.