1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri mkuu wa Urusi Dmitry Medvedev ajiuzulu

Angela Mdungu
15 Januari 2020

Waziri mkuu wa Urusi Dmitry Medvedev ametangaza kujiuzulu hii leo 15.01.2020 akisema kuwa yeye pamoja na serikali anayoiongoza inaachia ngazi ili kumpa nafasi Rais Vladmir Putin kufanya mabadiliko ya katiba

https://p.dw.com/p/3WFNp
Russland TV Interview Dmitri Medwedew
Picha: Getty Images/AFP/Sputnik/A. Astafyev

Medvedev ametoa tamko la kujiuzulu kupitia Televisheni ya Taifa ya Urusi akiwa ameketi sambamba na Rais Putin ambaye ni mshirika wake wa karibu. Kwa mujibu wa shirika la habari la Urusi,  Putin amemshukuru waziri mkuu huyo aliyejiuzulu kwa utumishi wake huku akibainisha kuwa baraza lake la Mawaziri lilishindwa kutimiza majukumu yake.

Medvedev ametumikia wadhifa huo wa uwaziri mkuu wa Urusi tangu mwaka 2012, kabla ya hapo alikuwa Rais wa nchi hiyo toka mwaka 2008 hadi 2012. Baada ya kujiuzulu kwa Medvedev na mawaziri wake Rais Putin ameliomba baraza hilo la mawaziri kuendelea kufanya kazi hadi hapo baraza jipya litakapotangazwa.

Tangazo la waziri mkuu wa Urusi ambalo halikutarajiwa  limetolewa muda mfupi baada ya Rais Putin  kutoa hotuba mapema leo akipendekeza kura ya maoni juu ya mabadiliko kadhaa kwenye katiba ya nchi yake, yatakayolipa bunge nguvu zaidi. Hatua hiyo huenda ikachochea uvumi juu ya hatma ya Putin baada ya kuwa madarakani kwa miaka 20. Hata hivyo kiongozi huyo wa Urusi hajadokeza chochote juu ya mipango yake ya nini kitakachofuata mara tu muhula wake wa uongozi utakapomalizika, mwaka 2024.

Russland Moskau Dmitry Medwedew (L) und Präsident Putin
Waziri mkuu wa Urusi Dmotry Medvedev akitangaza kujiuzulu. Kulia ni Rais Vladmir Putin Picha: Imago Images/Tass/A. Nikolsky

Ametoa mapendekezo hayo ya mabadiliko ya katiba  katika hotuba yake ya mwaka Ikiwa ni mwaka mmoja pekee uliosalia kuelekea uchaguzi wa bunge utakaofanyika mwaka 2021 huku chama tawala kikiwa kinakubalika kwa kiwango kidogo.

Baada ya kujiuzulu kwa Medvedev Urusi inahitaji waziri mkuu na baadhi ya wanaotajwa kushika wadhifa huo ni Sergei Sobyanin, Meya wa jiji la Moscow  Maxim Oreshkin, waziri wa Uchumi ama waziri wa nishati Alexander Novak.