1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ulaya yawakaribisha wakimbizi wa Ukraine

Mohammed Khelef
28 Februari 2022

Mamia kwa maelfu ya raia wa Ukraine wanakimbilia sasa kwenye mataifa jirani na wafikapo na kupokelewa na mapenzi ya wenyeji wao, lakini hivyo sivyo wanavyotendewa wakimbizi wanaokimbia madhila Mashariki ya Kati na Afrika

https://p.dw.com/p/47jTL
BdTD | Slowakei
Picha: Peter Lazar/AFP/Getty Images

Katika kuwapokea wakimbizi kutoka Ukraine, viongozi wa Poland, Hungary, Bulgaria, Moldova na Romania zinaelezea kwa uwazi tafauti iliyopo. Kwa mfano, Rais Rumen Radev wa Bulgaria aliwaambia waandishi wa habari mapema wiki hii kuhusu wakimbizi hao na hapa namnukuu: "Hawa sio wakimbizi tuliowazowea. Watu hawa ni Wazungu. Watu wenye akili, walioelimika. Hili si wimbi la wakimbizi tulilolizowea la watu ambao hatukuwa na uhakika wa utambulisho wao, watu wenye historia isiyo wazi, ambao wangeliweza kuwa magaidi." Mwisho wa kumnukuu.

Soma zaidi:Urusi yaiteka miji miwili midogo ya Kusini mwa Ukraine 

Kwa maneno ya rais huyo wa Bulgaria, hakuna nchi yoyote ya Ulaya inayoliogopa wimbi la sasa la wakimbizi kutoka Ukraine. Mwandishi wa habari wa Syria, Okba Mohammad, anasema japokuwa hajashangazwa kauli hii na nyengine kama hizi, inachanganya ubaguzi wa rangi na chuki dhidi ya Waislamu.

Polen ukrainische Flüchtlinge an der Grenze
Wakimbizi wa Ukraine waingia katika nchi za UlayaPicha: Omar Marques/Getty Images

Mohammad aliukimbia mji wake wa Daraa mwaka 2018. Hivi sasa anaishi nchini Uhispania, ambako kwa kushirikiana na wakimbizi wengine wa Syria wameasisi jarida la kwanza la lugha mbili za Kiarabu na Kihispania. Kama ilivyo maelfu ya Waukraini, naye pia alilazimika kujificha chini ya ardhi kujikinga na mabomu ya Urusi,. Naye pia alilazimika kupanda basi lililojaa abiria kuukimbia mji wake. Naye pia alitenganishwa na familia yake mpakani. Mohammad anasema, na hapa namnukuu: "Mkimbizi ni mkimbizi, awe Mzungu, Muafrika ama Muasia." Mwisho wa kumnukuu.

Soma pia: Baraza kuu la Umoja wa Mataifa kujadili Ukraine kwa dharura

Linapokuja suala la Ukraine, kauli za baadhi ya viongozi wa misimamo mikali ya kupinga wahamiaji barani Ulaya zimebadilika kutoka zile za "Hatutamruhusu yeyote kuingia" kuwa "Tunamruhusu kila mmoja kuingia." Kauli hizo zilitolewa kwa tafauti ya miezi mitatu tu na Waziri Mkuu wa Hungary, Viktor Orban. Ya kwanza, katika mwezi Disemba, alikuwa akizungumzia kuhusu wakimbizi na wahamiaji kutoka Mashariki ya Kati na Afrika wanaotaka kuingia Ulaya kupitia Hungary. Ya pili aliitowa wiki hii alipokuwa akizungumzia watu kutoka Ukraine.

Na sio wanasiasa pekee. Baadhi ya waandishi wa habari nao wanakosolewa kwa jinsi wanavyoripoti na kuwaelezea wakimbizi wa Ukraine. Kwa mfano, mtangazaji mmoja wa kituo cha televisheni cha Al Jazeera chenye makao yake makuu Doha, Qatar, alisema na hapa namnukuu: "Hawa sio tu wakimbizi wanaowania kukimbia maeneo ya Mashariki ya Kati, ama Afrika ya Kaskazini. Hawa wanaonekana kama familia yoyote ya Kizungu ambayo ungeliweza kuishi nayo kwenye nyumba ya jirani." Mwisho wa kumnukuu. Kituo hicho kimetowa tangazo la kuomba radhi kikisema kauli hiyo haikuzingitia hisia za watu na isiyo ya maana.

Karte mögliche Fluchtwege aus der Ukraine EN

Wakati watu zaidi ya milioni moja walipovuuka kuingia Ulaya mwaka 2015, uungaji mkono kwa wakimbizi wanaoikimbia vita nchini Syria, Iraq na Afghanistan ulikuwa mkubwa zaidi. Hapana shaka, kulikuwa pia na baadhi ya matukio ya uhasama - kama pale mpigapicha wa kike wa Hungary alipoonekana kwenye video akiwapiga mateke na kuwachania nguo wahamiaji katika mpaka wa nchi yake na Serbia.

Kansela wa wakati huo wa Ujerumani, Angela Merkel, alitowa kauli yake mashuhuri "Wir schaffen das" yaani "Tutalimudu hili" na waziri mkuu wa Sweden aliwataka raia "kufunuwa nyoyo zao kwa wakimbizi" hao. Wafanyakazi wa kujitolea kwenye fukwe za Ugirki kuziokowa familia ambazo zilikuwa zikiwasili kutoka Uturuki kwa mashua zisizo salama. Nchini Ujerumani, walipokelewa kwa sherehe katika vituo vya treni na mabasi.

Soma pia: Maoni: Hatimaye Ujerumani yaja na msimamo dhidi ya Urusi

Lakini, mapokezi hayo ya heshima na taadhima yalikoma ghafla baada ya mataifa ya Umoja wa Ulaya kutokukubaliana juu ya kugawana mzigo wa wakimbizi, ambapo shinikizo zaidi lilitoka mataifa ya Ulaya ya Kati na Mashariki kama Hungary na Poland. Moja baada ya nyengine, serikali barani Ulaya zikaimarisha sera za wahamiaji na waomba hifadhi na mbinyo mkali mipakani, uliopewa jina la "Ngome ya Ulaya".

AP