1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa zamani wa Afrika Kusini akana mashitaka ya rushwa

Bruce Amani
26 Mei 2021

Rais wa zamani wa Afrika Kusini Jacob Zuma ameyakana mashitaka ya rushwa, ulaghai na utakatishaji fedha kuhusiana na mpango wa ununuzi wa silaha kwa kiasi cha dola bilioni 2 wakati akiwa naibu rais.

https://p.dw.com/p/3tyon
Jacob Zuma | Korruptionsverfahren
Picha: Phill Magakoe/Reuters

Zuma, ambaye alikuwa rais kati ya 2009 na 2018, anakabiliwa na mashitaka 18 yanayohusiana na mkataba huo wa 1999.

Anakanusha mashitaka hayo akisema ni muathiriwa wa kampeni ya kisiasa ya kumchafulia jina inayofanywa na kundi pinzani katika Chama tawala cha African National Congress.

soma zaidi: Kesi ya ufisadi dhidi ya Zuma yaahirishwa

Zuma, anayekabiliwa na uchunguzi mwingine wa ufisadi uliofanywa wakati akiwa rais, anatuhumiwa kwa kukubali dola 34,000 kila mwaka kutoka kwa kampuni ya silaha ya Ufaransa Thales, ili nayo kampuni hiyo ilindwe dhidi ya uchunguzi kuhusiana na biashara hiyo.

Mawakili wa Zuma wanataka mwendesha mashitaka wa serikali Billy Downer aondolewe kwenye kesi hiyo, kwa misingi kuwa hana mamlaka ya kuongoza kesi hiyo. Upande wa mashitaka umeomba muda zaidi kujibu ombi hilo na uamuzi utafanywa Julai 19.