1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Morocco imeipiga Uhispania 3-0

Sudi Mnette
7 Desemba 2022

Morocco limekuwa taifa pekee la nne kwa Afrika kufuzu kuingia katika hatua ya robo fainali katika mchuano mkubwa wa kandanda duniani kwa kuitwanga Uhispania mabao 3-0 katika hatua ya mnyukano wa mikwaju ya penalti.

https://p.dw.com/p/4KZzr
Katar WM FIFA 2022 Achtelfinale Marokko vs Spanien Elfmeterschießen
Picha: ODD ANDERSEN/AFP

Hatua huyo ni baada ya kutoka sare ya bila ya kufungana baada ya muda wa nyongeza. Kipa wa Morocco Yassine Bounou, ambae pia anachezea klabu ya Sevilla ya Uhispania aliweza kupangua mikwaju miwili kati ya mitatu kutoka kwa timu hasimu.

Timu hiyo ambayo imecheza kiwango cha soka cha kuushangaza ulimwengu itakabiliana Ureno katika mchuano huo wa kombe la dunia katika ngwe ya timu nane zilizosalia. Na hatua hiyo ni baada ya Ureno kuichapa Uswisi mabao sita kwa moja. 

Wamoroko wameshuka katika miji mkubwa barani Ulaya kushangilia ushindi

Katar WM FIFA 2022 Achtelfinale Marokko vs Spanien Elfmeterschießen
Achraf Hakimi wa Morocco akifungaPicha: ODD ANDERSEN/AFP

Raia wa Morocco katika miji mbalimbali barani ulaya waliteremka mitaani katika kushanglia ushindi wa timu yao wa kihistoria, huku wakipeperusha bendera ya taifa lao. Kwa rekodi hiyo timu hiyo pia inakuwa ya kwanza katika ulimwengu wa soka wa mataifa ya kiarabu kufikia hatua ya robo fainali nchini Qatar.

Mfalme Mohammed VI, wa Morocco ameipongeza timu ya taifa akiijumuisha wachezaji, timu ya kiufundi na utawala mzima wa timu hiyo kwa kufanikiwa kufika hatua hiyo.

Ronaldo ashangilia ushindi wa timu yake Ureno akiwa mchezaji wa akiba

Katika ngwe nyingine ya michuano hiyo pamoja na nyota wake, Cristiano Ronaldo kusalia kuwa mchezaji wa akiba kwa muda mwingi, mbadala wake alifanikiwa kuweka katika muongozo wa ushidi timu yake ya Ureno dhidi ya Uswisi. Mshambuliaji Goncalo Ramos mwenye umri wa miaka 21 amefanya kazi njema uwanjani ambayo pengine ingepaswa kufanywa na Ronaldo.

Alifunga goli la kwanza katika dakika ya 17, na kuongeza mengine katika dakika za 51 na 67, katika kipindi ambacho mashabiki wa Ureno walikuwa wakimshangilia kwa jina la Ronaldo. Ronaldo mwenyewe mwenye umri wa miaka 37 aliingia kama mchezaji wa kiraka katika dakika ya 72.

Mayowe ya mashabiki yalizidi kuongezeka uwanjani ingawa ilionekana kama Ureno ilikuwa tayari ipo katika mkondo wa ushindi mkubwa kufuatia magoli yaliofungwa na beki Pepe, Raphael Guerreiro na baadae kabisa Rafael Leao.

Soma zaidi:Brazil imeifunga Korea Kusini, na Croatia Japan

Mfuta machozi wa Uswisi katika mchuano huo alikuwa Manuel Akanja, akifunga bao pekee. Kwa hatua hii sasa Ureno inaingia katika ngwe ya robo fainali kwa mara ya tatu baada ya 1966 na 2006. Na hivyo kukutana uso kwa uso na Morocco.

Kocha wa Ureno, Fernando Santos kwa wakati huu atakuwa na chaguo gumu la kuendelea kusalia na Ramos au kuendelea uwezo wa Ronaldo, mfungaji mkubwa katika soka la kimataifa na mmoja kati wachezaji wa hadhi ya juu kabisa katika tasnia hiyo.

Kwa kuweka rekodi katika michezo ijayo ya Ijumaa itakuwa Croatia na Brazil, Uholanzi na Argentina na siku inayofuata Jumamosi ambapo Morocco itafuana na Ureno na England na Ufaransa.

Vyanzo: AP/DPA