1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mamia ya Waislamu waandamana Kenya kupinga ushoga

7 Oktoba 2023

Mamia ya Waislamu wameandamana hapo jana nje ya jengo la Mahakama ya Juu ya Kenya jijini Nairobi, ili kupinga uamuzi wa mwezi uliopita wa kuthibitisha upya haki ya kujumuika kwa jamii ya mashoga.

https://p.dw.com/p/4XETG
Anti LGBTQ Protests I Kenya Gay Rights
Picha: Brian Inganga/AP/picture alliance

Waandamanaji hao wamesema "huu ni ukoloni mamboleo" na wamewataka baadhi ya majaji kutubu na kujiuzulu wakisema uamuzi huo unaunga mkono ukosefu wa maadili. Makundi ya kutetea haki za binadamu yamekemea maandamano hayo na kuyataja kuwa "hatari". 

Maandamano hayo yanafuatia uamuzi wa Mahakama ya Juu mwezi uliopita ulioruhusu watetezi wa haki za mashoga (LGBTQ) kujisajili kama shirika lisilo la kiserikali, uamuzi ambao umewakasirisha wahafidhina na kuchochea hotuba kali za kupinga ushoga.

Baada ya uamuzi huo,  Rais William Ruto alisema anaheshimu uamuzi wa Mahakama, lakini akabainisha pia kuwa utamaduni na dini nchini Kenya haviruhusu mahusiano ya jinsia moja.