1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yaamrisha kuondolewa kila mmoja Al-Shifa

18 Novemba 2023

Mamia ya watu wameikimbia hospitali ya Al-Shifa kwa miguu leo baada ya mkurugenzi wa hospitali hiyo kusema kwamba jeshi la Israel limetoa amri ya kuondolewa kwa watu katika kituo hicho cha afya.

https://p.dw.com/p/4Z83C
Mzozo wa Mashariki ya Kati - Hospitali ya Al-Shifa
Mhudumu akimhudumia mgonjwa hospitali ya Al-ShifaPicha: Saeed Jaras/APA/IMAGO

Wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas katika taarifa imesema watu wengine 120 waliojeruhiwa bado wako katika hospitali hiyo pamoja na idadi ambayo haijawekwa wazi ya watoto waliozaliwa kabla ya muda wao.

Mapema maafisa wa afya wa Hamas waliliambia shirika la habari la Ufaransa AFP kuwa watu 450 waliojeruhiwa na wagonjwa mahututi hawakuweza kuondolewa na wanasalia katika hospitali hiyo pamoja na wahudumu wa afya wanaowahudumia.

Wakati huo huo, huduma za intaneti na simu zimerejeshwa ingawa si kikamilifu katika Ukanda wa Gaza, na kufikisha mwisho kipindi cha kukatika kwa mawasiliano kilichoupelekea Umoja wa Mataifa kusitisha uwasilishaji wake wa misaada muhimu kwa kuwa misafara yake ya magari haikuweza kuwasiliana.

Hayo yanafanyika wakati ambapo shambulizi la anga la Israel nje kidogo ya eneo la Khan Younis limesababisha vifo vya watu 26.