1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel na Lebanon zakubaliana mipaka ya baharini

11 Oktoba 2022

Waziri mkuu wa Israel Yair Lapid amesema nchi yake imefikia makubaliano ya kihistoria na nchi jirani ya Lebanon kuhusu mpaka wa pamoja wa baharini. Hii ni baada ya miezi kadhaa ya majadiliano baina ya nchi hizo.

https://p.dw.com/p/4I382
Libanon I Marine Israel
Picha: Mohammed Zaatari/AP/picture alliance

Mkataba huo uliotangazwa unaashiria mafanikio makubwa kati ya nchi hizo mbili ambazo zimekuwa katika mzozo kwa zaidi ya miongo mitano iliopita.

Lakini mpango huo bado unakabiliwa na vizuizi, ikijumuisha changamoto muhimu za kisheria na kisiasa nchini Israel. Hata hivyo hakukuwa na uthibitisho wowote kutoka Lebanon juu ya kufikiwa kwa makubaliano hayo.

Hatarini ni haki juu ya uchimbaji wa hifadhi ya gesi asilia chini ya bahari katika maeneo ya mashariki mwa bahari ya Mediterania ambayo nchi hizo mbili zisizo na uhusiano wa kidiplomasia, zinagombania.

Waziri Mkuu Yair Lapid aliuita mpango huo ``mafanikio ya kihistoria yatakayoimarisha usalama wa Israel, kuingiza mabilioni katika uchumi, na kuhakikisha uthabiti wa mpaka wa kaskazini.''

Israel Verteidigungsminister Benny Gantz
Waziri wa masuala ya ulinzi Israel Benny GantzPicha: GPO/AA/picture alliance

Waziri wa masuala ya ulinzi Israel Benny Gantz, amenukuliwa na vyombo vya habari akisema Israel ina haki ya kuwa na mashirikiano na Lebanon kama jirani thabiti na wa kutegemea na anayenufaika na makubaliano hayo ambayo yananuia kunufaisha pande zote mbili.

Benny Gantz, amesema "Tumedhamiria kuhakikisha kwamba makubaliano hayo yanalinda maslahi ya usalama ya Taifa la Israel. Hatutasalimisha hata 'milimita' moja ya usalama wetu. Makubaliano hayo yanaendelea licha ya vitisho vya kundi la kigaidi la Hezbollah ambalo lilijaribu kuhujumu mchakato huo, na sio kwa sababu yake. Tutaendelea kusisitiza juu ya mahitaji yetu ya usalama katika hali yoyote na kutoa usalama kwa raia wa Israeli."

Dhima ya makubaliano hayo

Leviathan Gasfeld im Mittelmeer vor Haifa
Picha: Amir Cohen/REUTERS

Mbali na mambo mengine mkataba huo una dhima ya kuwezesha uzalishaji wa ziada wa gesi asilia katika bahari ya Mediterania. Baadhi ya wachambuzi wanasema makubaliano hayo yanakabiliwa na vikwazo kadhaa ikiwemo vya kisheria na kisiasa nchini Israel.

Kulingana na afisa mkuu wa Israel, Lebanon itaruhusiwa kuzalisha gesi kutoka katika eneo linaloitwa ``Qana,'' lakini kuilipa Mirahaba Israeli kwa gesi yoyote inayozalishwa kutoka upande wa Israel. Lebanon imekuwa ikifanya kazi na kampuni kubwa ya nishati ya Ufaransa ya Total juu ya maandalizi ya uzalishaji gesi.

Kwa mujibu wa Afisa wa mmoja wa Israel aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina ili kujadili sera za serikali amesema mpango huo utafikishwa mbele ya Baraza la Usalama na Baraza la Mawaziri kisha utawasilishwa Bungeni kwa mapitio ya siku 14. Baada ya ukaguzi, Baraza la Mawaziri litakutana tena ili kutoa idhini ya mwisho, rasmi.

 

/AP