1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Harry Maguire aitwa tena kwenye kikosi cha England

20 Machi 2026

England imemuita beki wake Harry Maguire kwenye mechi za kirafiki za mwezi huu dhidi ya Uruguay na Japan.

https://p.dw.com/p/5AnLz
UEFA Europa League | Sevilla dhidi ya Manchester United
Harry Maguire (katikati) ameitwa tena kwenye kikosi cha taifa cha England wakati inapojiandaa na mechi za kirafiki kuelekea Kombe la DuniaPicha: Kieran McManus/Shutterstock/IMAGO

Meneja wa England Thomas Tuchel ametangaza kikosi cha wachezaji 35, Ijumaa wakati timu yake ikiendelea na maandalizi ya Kombe la Dunia.

Harry Maguire, ambaye amecheza mechi 64, aliichezea England mara ya mwisho mwaka wa 2024 na alikuwa kwenye kikosi kilichokosa ubingwa wa Ulaya wa 2024, ambapo England ilimaliza ikiwa ya pili.

Hata hivyo, nyota ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 33 imeng'ara tena baada ya kuitwa na hasa kutokana na kiwango cha sasa cha Manchester United iliyofufuka hivi karibuni, pamoja na mchezaji mwenzake Kobbie Mainoo.

"Harry anastahili. Amekuwa akicheza vizuri sana, hasa tangu Michael Carrick achukue nafasi yake, na kuwa na matokeo mazuri sana," Tuchel alisema.

Beki wa AC Milan, Fikayo Tomori, aliyeichezea England mara ya mwisho mwaka 2023, na mshambuliaji wa Leeds United, Dominic Calvert-Lewin, ambaye alicheza mara ya mwisho mwaka 2021, wote wamejumuishwa katika kikosi hicho.

Kocha wa England | Kombe la Dunia | Thomas Tuchel
Kocha wa England Thomas Tuchel amemuita tena Harry Maguire kwenye kikosi cha timu ya taifa Picha: Glyn Kirk/AFP

England kuwakaribisha Uruguay Wembley

England itawakaribisha Uruguay katika Uwanja wa Wembley Machi 27, ikifuatiwa na mchezo na Japan katika uwanja huo huo siku nne baadaye. Tuchel alisema ametangaza kikosi kikubwa hivyo kwa sababu angewagawanya wachezaji katika vikosi viwili tofauti kwa michezo hiyo miwili.

Kiungo wa kati wa Everton James Garner na kipa wa Brighton & Hove Albion Jason Steele waliitwa kwa mara ya kwanza, huku kipa huyo akitarajiwa pia kujiunga na kikosi cha Kombe la Dunia kama kipa wa mazoezi.

Kiungo wa kati wa Real Madrid, Jude Bellingham ambaye amekuwa nje kwa wiki kadhaa kutokana na jeraha la misuli ya paja, pia aliitwa, lakini beki Trent Alexander-Arnold hakupata nafasi.

England pia imepangwa kucheza mechi za ziada dhidi ya New Zealand na Costa Rica mwezi Juni kama sehemu ya maandalizi ya Kombe la Dunia, litakaloandaliwa na Marekani, Canada na Mexico

England iko katika Kundi L la Kombe la Dunia, ambapo watakabiliana na Croatia, Ghana na Panama katika hatua ya makundi. Mechi yao ya ufunguzi imepangwa kufanyika Juni 17 dhidi ya Croatia mjini Dallas

Timu ya Taifa - England
Timu ya Taifa ya England iliyocheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Brazil kwenye uwanja wa Wembley, LondonPicha: Action Foto Sport/NurPhoto/picture alliance

KIKOSI

Walinda lango: Dean Henderson, Jordan ​Pickford, James Trafford, Aaron Ramsdale, Jason Steele

Walinzi: Dan Burn, Marc Guehi, Lewis Hall, Ezri Konsa, Tino Livramento, Harry Maguire, Nico O'Reilly, Jarell Quansah, Djed Spence, John Stones, Fikayo Tomori

Viungo: Elliot Anderson, Jude Bellingham, James Garner, Jordan Henderson, Kobbie Mainoo, Declan Rice, Morgan Rogers, Adam Wharton

Washambuliaji: Jarrod Bowen, Dominic Calvert-Lewin, Eberechi Eze, Phil Foden, Anthony Gordon, Harry Kane, Noni Madueke, Cole Palmer, Marcus Rashford, Bukayo Saka, Dominic Solanke