1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Cyprus yapeleka suala la mvutano wa kisiwa mbele ya UN

Tatu Karema
21 Julai 2021

Mvutano wa kisiwa cha Cyprus kilichogawika umechukua mwelekeo mpya baada ya Cyprus ya upande wa Uturuki kuchukua sehemu ya mji wa Varosha uliotelekezwa miaka 47 iliyopita kwa lengo la kuanzisha makaazi ya raia wake.

https://p.dw.com/p/3xo1s
Zypern Ansprache Präsident Nicos Anastasiades
Picha: picture-alliance/AP Photo/P. Karadjias

Kwa mujibu wa waziri wa mambo ya nje wa Serikali ya Cyprus iliyoko mjini Nicosia inayotambulika kimataifa imelipeleka suala la mvutano wa kisiwa hicho mbele ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa, kuhusiana na suala la kuchukuliwa kwa sehemu ya mji wa pwani uliotelekezwa miaka 47 iliyopita wa Varosha na Cyprus ya Uturuki. Maafisa wa Cyprus ya Uturuki na Uturuki yenyewe jana Jumanne walitangaza kwamba sehemu ndogo ya mji huo wa Varosha  itakuwa chini ya mamlaka ya raia kwa ajili ya uwezekano wa kuanzisha makaazi mapya. Lakini waziri wa mambo ya nje wa Jamhuri ya Cyprus Nikos Christodoulides wakati alipokutana na mwenzake wa Ugiriki Nikos  Dendias alisema hatua hiyo ni ukiukaji wa wazi wa maazimio ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa na itakuwa na athari mbaya katika juhudi zinazoendelea za kuanzishwa mazungumzo ya kutafuta mwafaka kuhusu mvutano wa kisiwa hicho.Kwa upande wake Dendias amesema alisema kuwa hakuna nafasi ya kuimarika kwa uhusiano kati ya Umoja wa Ulaya na Uturuki wakati Uturuki ikiendeleza hatua zinazokiuka sheria nchini Cyprus na kwaba hayo yametajwa katika maamuzi ya baraza la Ulaya.

Charbel Wehbe | libanesischer Außenminister
Waziri mkuu wa Ugiriki- Nikos DendiasPicha: Giannis Panagopoulos/ANE/Eurokinissi/picture alliance

Wacyprus wa upande wa Ugiriki ambao ndio wanawakilisha kisiwa chote cha Cyprus kimataifa wanahofia mabadiliko ya mji huo yanaonesha wazi dhamira ya Cyprus ya Uturuki iliyojitenga pamoja na washirika wake Uturuki ya kutaka kuumiliki mji huo. Hatua ya Cyprus ya Uturuki pia imechochea sauti za kuikosoa kutoka nchi za Magharibi zikiongozwa na Marekani ambayo imesema kitendo hicho hakikubaliki na ni cha uchokozi. Waziri wa mambo ya nje wa Ugiriki Nikos Dendias amesema hatua iliyochukuliwa jana na upande wa Cyprus ya Uturuki ni ya kujaribu kutengeneza mvutano mpya kuzika kabisa matumaini ya kukiunganisha kisiwa hicho.

Ikumbukwe kwamba mji wa Varosha umetekelezwa tangu vita mwaka vya 1974 vilivyokigawa kisiwa hicho cha Cyprus kwa misingi wa kikabila. Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa linatarajiwa kujadili suala hilo Jumatano katika mkutano ambao awali ulipangwa kuzungumzia shughuli zake katika kisiwa hicho. Baraza la Usalama limekuwa likijaribu bila ya mafanikio kwa kipindi cha miongo kukiunganisha kisiwa hicho tangu vita hivyo vya 1974 vilivyosababishwa na uvamizi wa Uturuki baada ya mapinduzi yaliyofanywa katika Cyprus ya Ugiriki yaliyoanzishwa na jeshi lililokuwa wakati huo likiitawala Ugiriki.