1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DRC yaongeza muda wa hali ya dharura mikoa ya mashariki

John Kanyunyu4 Juni 2021

Bunge la Congo limeongeza muda wa dharura katika mikoa ya Kivu Kaskazini na Ituri. Hata hivyo kupitishwa kwa sheria hiyo kunafanyika wakati wakaazi wa mikoa hiyo bado hawajaona mabadliliko, kwani mauaji bado yanaendelea

https://p.dw.com/p/3uQr6
Demokratische Republik Kongo | Mai-Mai-Milizen
Picha: Phil Moore/AFP/Getty Images

Wakizungumza na DW, baada ya bunge kupitisha sheria kuhusu kuongezwa muda wa ziada hali ya dharura katika eneo hili, wakaazi wa Beni walisema kwamba wanashangaa kuona wabunge wanapitisha sheria hiyo, bila hata kutathimini kilichofanywa na magavana wa kijeshi, tangu kuteuliwa kwao mwezi moja sasa.

Tangu kutangazwa kwa hali ya dharura katika mikoa ya Kivu Kaskazini pamoja na Ituri, mashambulizi ya makundi ya waasi yameshika kasi, na kwa kipindi cha wiki moja pekee, waasi hao wamewauwa watu wasiopungua mia mbili, katika vijiji mbalimbali vya mikoa miwili inayohusika na machafuko.

Soma pia: Mauaji ya waasi wa ADF nchini DRC kupata suluhu?

Hivi karibuni, waasi hao walikishambulia kijiji cha Mayimoya na kuwauwa watu wanane, huku wengine wengi wakitekwa nyara na kundi la waasi wa ADF, wakiwemo mwalimu wa kike, pamoja na baadhi ya wanafunzi wake.

DR Kongo Militärischer Gouverneur von Nord-Kivu Constant Ndima
Gavana wa kijeshi wa Kivu Kaskazini Constant Ndima.Picha: Benjamin Kasembe/DW

Akizungumza na DW kwa njia ya simu, mwenyekiti wa mashirika ya kiraia katika Kongamano la Bambuba Kisiki, Patrick Musubaho amesema kwamba kuna raia zaidi ya hamsini waliotoroka baada ya kutekwa na ADF katika eneo la Tsanitsani.

Hatua ya hali ya dharura inaongezewa muda baada ya kuchukuwa uongozi, kamanda mpya wa operesheni dhidi ya waasi, na kubwa katika yote likiwa ni lile la ADF kutoka Uganda.

Soma pia: DRC: Chuo cha mafunzo ya kivita chazinduliwa

Hadi sasa Mameya wa kijeshi wa miji ya Beni na Butembo, pamoja na tarafa mbalimbali wa miji hiyo, hawajawasili katika maeneo wanakotakiwa kufanya kazi, baada ya kuteuliwa na rais karibu wiki mbili sasa, na wakiwa wanabaki na siku kumi na tano tu za kuchapa kazi.