1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baraza la Usalama la UN kukutana kuijadili Libya

Zainab Aziz
15 Julai 2021

Waziri wa Mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas atahudhuria mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu mzozo wa Libya leo hii Alhamisi.

https://p.dw.com/p/3wWIn
Schweiz Libysches Dialogforum in Genf
Picha: UNITED NATIONS/AFP

Wajumbe wa baraza hilo watajadili matokeo ya mkutano wa kimataifa uliofanyika mjini Berlin, Ujerumani wiki tatu zilizopita, ambao kwa mara nyingine ulilenga kukomesha uingiliaji wa kigeni katika mzozo wa Libya.

Washiriki ambao ni pamoja na Urusi, Uturuki na Misri waliahidi kuwaondoa wapiganaji wote wa kigeni kutoka kwenye nchi hiyo ya Kaskazini mwa Afrika ingawa bado haijathibitika iwapo wapiganaji hao wameondolewa na iwapo zoezi hilo litafanyika katika siku za hivi karibuni.

Soma pia: Umoja wa Ulaya wataka wapiganaji mamluki kuondoka Libya

Kulingana na makadirio ya hivi karibuni ya Umoja wa Mataifa, vikosi vya askari wa kigeni wapatao 20,000 bado wanatumika nchini Libya lhadi hii leo.

Matokeo ya pili muhimu ya mkutano huo wa Berlin, ni kuunga mkono uchaguzi utakaofanyika tarehe 24 Desemba ambapo mpaka sasa mahitaji yote bado hayajatimizwa.

Serikali ya mpito iliundwa chini ya upatanishi wa Umoja wa Mataifa na jukumu lake ni kuiongoza nchi hiyo hadi wakati wa kufanyika uchaguzi lakini Libya bado ina changamoto kwani hakuna misingi ya kisheria nchini humo hadi sasa.