1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Asasi za kiraia kutoridhishwa na tathmini kuhusu Loliondo

Veronica Natalis26 Januari 2023

Mashirika yanayohusika na utetezi wa haki za jamii yanadai hayajaridhishwa na mwenendo wa makamishna waliokwenda kutathimini hali ya ukiukwaji wa haki za binadamu eneo la Loliondo na Ngorongoro.

https://p.dw.com/p/4MiD2
Familia za Wamasai wasio na makao baada ya vibanda vyao kuteketezwa
Familia za Wamasai wasio na makao baada ya vibanda vyao kuteketezwaPicha: DW/C.Ngereza

Katika barua yao, mashirika hayo nane yaliyopo Arusha kaskazini mwa Tanzania  yamebainisha kwamba hayajaridhishwa na jinsi zoezi hilo lilivyofanyika kwani makamishina wa tume hiyo ya haki za binadamu Afrika yenye makao yake makuu mjini Banjul Gambia, hawakuwa huru kukutana na wahanga halisi, bali maafisa wa serikali ya Tanzania walikuwa nao bega kwa bega na kuwatafutia watu wa kukutana na kuzungumza nao.

Kulingana na barua hiyo, uwepo wa maofisa wa serikali wakati wa mahojiano na tume, pamoja na ratiba yao kutotoa nafasi ya kukutana na wanananchi na azaki, kulifanya azaki kusikilizwa kwa njia ya dharura kutegemeana na muda na ratiba iliyopangwa na serikali. Wakili Denis Olushangai ni mwakilishi wa mashirika hayo.

Kwa upande mwingie baadhi ya wakaazi wa tarafa ya Loliondo na Ngorongoro ambao ndio wanatajwa kuwa waathirika wakubwa wa uvunjifu wa haki za binadamu wanasema hawakupata nafasi yakutoa maoni yao na kwa jumla  hawakuwa na taarifa za ujio wa tume hiyo.

Serikali yatupilia mbali madai ya uvunjifu wa haki

Wananchi wa jamii ya Wamasai wakijaribu kupata maji kwa ajili ya mifugo yao
Wananchi wa jamii ya Wamasai wakijaribu kupata maji kwa ajili ya mifugo yaoPicha: DW/A. Mittal

Pamoja na mambo mengine mashirika hayo pia yanashinikiza kuwekwa wazi kwa tarehe ambayo makamishina hao wa tume watazungumza na vyombo vya habari ili kutoa fursa kwa vyombo huru vya habari kuhudhuria.

Hata hivyo serikali ya Tanzania imekuwa ikikanusha vikali madai ya uvinjifu wa haki za binadamu katika maeneo hayo ambapo mwaka jana naibu waziri wa katiba na sheria wa Tanzania Godfrey Pinda, alikwenda mjini Banjul Gambia yalipo makao makuu ya tume ya Afrika ya haki za binadamu, na alinukuliwa akisema kuwa hakuna ukiukwaji wa haki za binadamu hasa hasa haki za wa jamii ya wafugaji wa Masai wa Loliondo na Ngorongoro.