1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Usugu wa antibayotiki na inapogeuka kuwa sumu

Iddi Ssessanga
20 Novemba 2023

Tarehe 18 mpaka 24 mwezi huu wa Novemba ni wiki ya uhamasishaji juu ya matumizi sahihi ya dawa za kutibu maambukizi ya bakteria - maarufu kama Antibayotiki, na sababu zinaozoweza kusababisha usugu wa dawa hizo.

https://p.dw.com/p/4ZEYa
Afya | Bakteria wanavyoweza kujigawa kwa kutumia vinasaba
Afya | Picha inaonesha namna bakteria wanavyoweza kuhama kwa kutumia vinasabaPicha: Science Photo Library/IMAGO

Katika ulimwengu usio na anti-biotics, magonjwa tunayoyatibu kwa urahisi hii leo yanaweza kugeuka tishio la maisha, kutokana na bakteria zaidi kujenga usugu dhidi ya dawa za kawaida. Hebu fikiria kwa mfano, kwamba una maambukizi kwenye njia ya mkojo, UTI.

Mwanzoni unaweza kuwa wasiwasi tu, lakini kwa haraka hali inageuka kuwa maumivu makali, ambayo hayawezi kutulizwa kwa kulala chini na kujikanda na kunywa maji mengi.

Lakini kuna njia rahisi; Unaenda kwa daktari wako na kupata dawa ya kutibu maambukizi ya bakteria.

Soma pia:Ripoti: Vimelea vya Malaria vimekuwa sugu

Dalili zako zinaweza kutoweka ndani ya siku tatu hadi tano baada ya kuanza kumeza vidonge hivyo vidogo. Haya ndiyo maajabu ya tiba za kisasa.

Lakini hebu sasa fikiria hali ambapo hakuna dawa hizo! Maambuzi yanaweza kusambaa kwenye figo zako, au kuingia kwenye mzunguko wako wa damu. Maisha yako yangekuwa hatarini.

Maisha bila antibayotiki yanawezekana?

Ulimwengu usiyo na dawa za kutibu maambukizi ya bakteria siyo ulimwengu mbadala au filamu ya kutisha. Ni hali inayotukabili sasa hivi.

Bakteria zaidi na zaidi wanakuwa sugu kwa dawa zilizotengenezwa kutibu maambukizo yanayosababishwa na bakteria hawa.

Wazo la msingi ni kuua bakteria kwa antibiotics. Lakini kuna uwezekano kwamba bakteria hao wataishi na kuwa sugu.

Afya | kasha la dawa
Afya | Dawa aina ya Amoskilini kwa ajili ya watotoPicha: Joly Victor/ABACA/picture alliance/dpa

Kuwa na antibiotic zisizofanya kazi tena na sawa na kutokuwa na antibiotic kabisaa.

Mnamo mwaka 2019, karibu watu milioni 1.27 kote duniani walikufa kutokana na maambuzi ya bakteria wasiosikia tena dawa, kulingana na utafiti uliochapishwa katika jarida la kitabibu la The Lancet.

Kituo cha Ulaya cha Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa kinakadiria kwamba Ulaya hushuhudia zaidi ya maambukizo 670,000 na bakteria sugu wasiosikia dawa kila mwaka, na kwamba takriban watu 33,000 katika bara hilo hufa kila mwaka kutokana na tatizo hilo.

Soma pia:Uganda: Ruksa wasichana wadogo kutumia uzazi wa mpango

Wataalamu wa matibabu wanazidi kuwa na wasiwasi kuhusu kupungua kwa ufanisi wa dawa zetu nyingi zinazoaminika.

Chris Dowson, aliefanya utafiti juu ya usugu wa dawa za antiobiotic kwa miongo kadhaa na ndiye mkuu wa kundi la utafiti wa magongwa ya kuambukizwa katika chuo kikuu cha Warwick cha nchini Uingereza, anasema dawa hizo zitaacha kufanya kazi na hivyo kuna haja ya kutafuta mbadala.

Lakini je, tumefikaje hapa? Kwanini kuna bakteria wengi wasioweza kuuawa kwa matibabu ya dawa zetu tena?

Usugu umeongezeka pakubwa katika miaka iliyopita kutokana na matumizi yaliopitiliza ya antibiotics.

Madaktari huwaandikia wagonjwa dawa hizo kwa urahisi zaidi kuliko hapo awali, ikiwa ni pamoja na katika hali ambapo inaweza kuwa siyo lazima.

Na wakati mwingine wagonjwa huacha kutumia dawa zao za antibiotic wanapojisikia nafuu ― licha ya madaktari kusema wagonjwa wanapaswa wakati wote kutumia dozi nzima ya antibiotics.

Kwanini ni rahisi kukatisha dozi za Antibayotiki?

Sababu ni rahisi: Mgonjwa anaweza kujisikia vizuri, lakini maambukizi yanaweza kuwepo bado, na kwa sababu haujameza dozi kamili, inaweza kuwa haitoshi kuua bakteria wote.

Hapo ndipo bakteria hupata nafasi ya kupambana kushinda kiwango cha chini cha antibiotics na kuzowea.

Na katika baadhi ya nchi, unaweza kupata antibiotics bila maelezo ya daktari, jambo ambalo huongeza uwezekano wa matumizi mabaya. Sababu zote hizi huchangia bakteria kuwa sugu kwa dawa zilizokuwa zikiwaua hapo awali.

Wakati gani wa kutumia antibiotiki na wakati gani hupaswi?

Katika kilimo, dawa za antibiotic hunyunyizwakwenye matunda bustani ili kuzuia wadudu, au hulishwa kwa wanyama katika uzalishaji mkubwa wa nyama. Kwa njia hii, antibiotics huingia kwenye maji yetu na chakula chetu.

Viwango vya antibiotics wanavyokutana navyo bakteria havitoshi kuwaua, na badala yake hufanya kazi kama nyenzo za mafunzo: Bakteria hujifunza kutoka kwao na kubadilika ili kuwa sugu.

Soma pia:Dawa za kusisimua misuli: Paul Pogba asimamishwa kwa muda

Kwa mujibu wa shirika la afya duniani, WHO, idadi ya maambukizi yanayosababishwa na bakteria wasiosikia dawa imeongezeka kwa asilimia 15 kutoka mwaka 2017 hadi 2021.

Bakteria wanaosababisha maambukizzi kwenye njia ya mkojo wanazidi kuwa sugu pia. Kifua kikuu pia kinazidi kuwa kigumu kutibu kwa sababu ya usugu wa dawa.

Watafiti kutoka nchini Ujerumani na Msumbiji waligundua kuwa  kuna vimelea vya kifua kikuu vinavyosambaa nchini Msumbiji ambavyo haviskii dawa, ambazo WHO inazipendekeza kwa matibabu.