1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Amnesty: Waandamanaji 12 wameuwawa Nigeria

22 Oktoba 2020

Shirika la haki za binadamu la kimataifa, Amnesty International, limesema katika ripoti kuwa vikosi vya usalama vya Nigeria vilifyatua risasi na kuwauwa watu 12 waliokuwa wanaopinga ukatili wa polisi.

https://p.dw.com/p/3kGwv
Nigeria Demo gegen Polizeigewalt in Lagos
Picha: Olukayode Jaiyeola/NurPhoto/picture-alliance

Katika ripoti iliyotoleqwa siku ya Jumatano, Amnesty imesema vikosi vya usalama vya Nigeria vilifyatua risasi katika mikusanyiko miwili mikubwa ya maandamano ya amani, Jumanne usiku, na kuuwa watu 12.  

Shirika hilo limesema watu wasiopungua 56 wamefariki katika wiki mbili za maandamano dhidi ya vurugu za polisi, wakiwemo 38 siku ya Jumanne.

Mzozo wa unaozidi kuchacha nchini Nigeria umevutia nadhari ya kimataifa, na kulaaniwa na watu mashuhuri, akiwemo katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres na mgombea wa chama cha Democratic nchini Marekani Joe Biden.

Akilaani vurugu za polisi katika mahojiano na shirika la habari la Associated Press, katibu mkuu wa UN Guterres alisema.

"Wakati umefika kwa mataifa kuelewa, na natumai Nigeria itaweza kufanya hivyo, kwamba ukatili wa polisi unahitaji kukomeshwa na wale wanaohusika na vitendo vya vurugu wanwajibishwe. Na hili ni muhimu kila mahala."

Nigeria Abuja | Aussschreitungen
Picha: Kola Sulaimon/AFP/Getty Images

Wakati huo huo, mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Josep Borrel pia alilaani mauaji ya waandamanaji akitoa wito wa kupatikana haki. Umoja wa Mataifa na Umoja wa Ulaya zimeitaka mamlaka nchini Nigeria kuchunguza na kuwawajibisha waliohusika na matukio hayo.

Rais wa Nigeria Muhammadu Buhari, ambaye amezungumzia kwa uchache sana juu ya maandano hayo, alitoa taarifa jana na kutoa wito wa utulivu

Serikali ya Nigeria bado haikutoa tamko lolote kuhusu madai hayo ya Amnesty International.

Maandamano hayo yalianza kama wito kwa serikali ya Nigeria kukifunga kikosi maalum cha polisi cha kupambana na ujambazi, SARS kwa madai ya kutumia nguvu kupindukia.

Lakini maandamano hayo yamekuwa makubwa zaidi na sasa yanadai pia utawala bora nchini Nigeria.