1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

AfD cha Ujerumani kutajwa kama kundi la itikadi kali?

Lilian Mtono
12 Machi 2024

Chama Mbadala kwa Ujerumani, AfD kinasubiri maamuzi ya kesi dhidi yake iliyowasilishwa na idara ya upelelezi wa ndani, BfV. Je, pengine chama hiki kitachunguzwa kama kundi linaloshukiwa kuwa lenye itikadi kali?

https://p.dw.com/p/4dQtk
Waandamanaji wanaokipinga chama cha AfD wakiandamana katikati ya mji wa Frankfurt
Mwandamanaji akiwa amenyanyua bango lenye ujumbe wa kukipinga chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha AfD nchini UjerumaniPicha: Kirill Kudryavtsev/AFP/Getty Images

Kwa miaka mingi, chama hicho cha kisiasa Mbadala kwa Ujerumani, AfD na idara hiyo ya upelelezi wa ndani, BfV, yenye jukumu la kuilinda katiba, wamekuwa wakipambana mara kadhaa mahakamani, na hoja kubwa ikiwa ni kama BfV ina uwezo wa kisheria wa kukichunguza chama kinachoshukiwa kufanya shughuli zinazokinzana na katiba.

Mnyukano wa sasa wa kisheria unashuhudiwa katika Mahakama ya Juu zaidi ya Kiutawala, OVG iliyoko mjini Münster mnamo kuanzia Machi 12 hadi 13.

Soma pia:Mahakama Ujerumani yapiga marufuku chama cha itikadi kali cha Heimat kupokea ruzuku ya serikali 

AfD inapinga uamuzi uliotolewa mwaka 2021 ulioagiza chama hicho kuchunguzwa kutokana na madai ya kuwa na itikadi kali za mrengo wa kulia na hasa kutokana na misimamo yake mikali iliyoibua mashaka.

Wakati huo, idara hiyo ya upelelezi ingeweza kuchukua hatua zaidi kuliko taasisi yoyote ile kwa kuzingatia machapisho kwenye magazeti, mitandaoni, ripoti zilizorushwa kwenye vituo vya televisheni na kwenye intaneti, kusikiliza hotuba zilizotolewa na wanachama wa AfD bungeni na hata kwenye makongamano ya chama hicho na kuyatumia.

Ikiwa rufaa ya AfD itafanikiwa, basi chama hicho hakitachunguzwa zaidi.

AfD kinashutumiwa kwa kuwa na misimamo ya kupinga wageni
Idara ya upelelezi wa ndani nchini Ujerumani, BfV inaangazia kuendelea kukichunguza chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha AfDPicha: Christoph Hardt/Geisler-Fotopress/picture alliance

Wakati huo huo, BfV inakusudia kwenda mbali zaidi kwa kukiainisha chama cha AfD kama kundi la "mrengo wa kulia wenye msimamo mkali" katika ngazi ya shirikisho, badala ya kuliacha kuwa suala la kuchunguzwa kwa muda mrefu ili kuthibitisha ukweli.

Mjadala juu ya kukizuia chama cha AfD

Hivi sasa wanachama waliothibitishwa kama wenye misimamo mikali huenda wakafuatiliwa zaidi na idara za upelelezi kuliko wakati wowote ule.

Soma pia: Hofu ya "fashisti" kuongoza serikali ya jimbo Ujerumani

Na ikiwa AfD itashindwa kwenye rufaa hii, huenda shinikizo la kukipiga marufuku chama hicho likaanza. BfV, tayari imeainisha mahitaji maalumu ikiwa shinikizo hilo litaanzishwa, ikiwa ni pamoja na kuweko vielelezo thabiti vinavyothibitisha kwamba chama hicho kina lengo la kushambulia na kuuondoa utaratibu wa uhuru na wa kidemokrasia wa nchini Ujerumani.

Kumekuwepo na maandamano nchini Ujerumani ya kukipinga chama cha AfD
Maneno kama yanavyoonekana kwenye bango hilo yakisema "AfD kipigwe marufuku mara moja". Chama hicho kinapingwa kutokana na misimamo yakePicha: Christian Ditsch/epd/IMAGO

AfD kunyimwa fedha za kodi?

Kisheria, ni Mahakama ya Katiba ya Shirikisho inayotakiwa kutoa uamuzi wa ikiwa chama kinaweza kupigwa marufuku au la. Ombi la zuio linaweza kuwasilishwa na serikali ya shirikisho, Bundestag ama Bundesrat.

Muungano wa vyama tawala katika jimbo la Bremen vya Social Democrats, SPD, Kijani na cha Kushoto unajiandaa kuchukua hatua hiyo.

Soma pia: AfD yaongoza dhidi ya CDU jimboni Saxony kuelekea uchaguzi wa Septemba

Hata hivyo, Wajerumani wengi wana mashaka: Kwa mfano utafiti wa taasisi ya Infratest.dimap kwa mwaka huu wa 2024, asilimia 51 hawaungi mkono chama hicho kupigwa marufuku.

Lakini namna nyingine ya kudhoofisha uthabiti wa chama hicho itakuwa ni kukiondolea stahiki ya kupata ufadhili kutoka serikalini. Ufadhili huu ndio chanzo kikubwa cha mapato kwa vyama vingi, ukiachilia mbali ada na michango ya wanachama.

Na hata ikiwa hili litawezekana, swali ambalo bado linasalia miongoni mwa wafuatiliaji wa mambo ni kama hata kuna huo uwezekano wa kukipiga marufuku chama hicho.

Sikiliza zaidi:

Mahojiano: Hasira za Wajerumani kwa AfD zinamaanisha nini?