1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 85 wauawa Gaza kufuatia mashambulizi ya Israel

19 Septemba 2025

Mamlaka za Gaza zimesema watu wasiopungua 85 wameuawa katika Ukanda wa Gaza katika kipindi cha saa 24 zilizopita.

https://p.dw.com/p/50icO
Gaza | Kifaru cha jeshi la Israel kikijiandaa kwa mashambulizi
Kifaru cha jeshi la Israel kikiingia Gaza kufanya mashambuliziPicha: Menahem Kahana/AFP/Getty Images

Aidha Israel imeendeleza operesheni yake ya kijeshi katika jiji la Gaza huku maelfu ya Wapalestina wakiendelea kuondoka katika jiji hilo. Mashambulizi hayo yamepelekea kukatika kwa umeme na mawasiliano ya simu na intaneti.

Hayo yakiarifiwa, Marekani kwa mara nyingine tena imetumia kura yake ya turufu hapo jana Alhamisi na kuzuia kupitishwa kwa azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lililotaka kusitishwa kwa mapigano huko  Gaza , kuwezesha ufikiaji wa misaada ya kibinadamu na kuachiliwa kwa mateka.

Azimio hilo liliungwa mkono na wanachama wote 14 wa baraza hilo ispokuwa Marekani ambayo ilipendekeza uwepo wa azimio la kibinaadamu pekee. Lakini Ufaransa, Uingereza na Urusi zilitilia shaka faida na ufanisi wa azimio la kibinadamu pekee kutoka kwa chombo kilichoundwa kwa ajili ya kudumisha amani na usalama duniani.