1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapalastina waandamana kuikumbuka siku ya Naqba

Oumilkheir Hamidou
15 Mei 2019

Naqba, ya kuikumbuka siku malaki ya wapalastina walipolazimishwa kuyahama maskani yao mwaka 1948 yamefanyika Gaza na katika ukingo wa magharibi wa mto Jordan

https://p.dw.com/p/3IYMe
Gazastreifen Grenze Israel Freitagsproteste
Picha: picture-alliance/Photoshot

Maelfu ya watu wameteremka katika eneo la mpaka unaoitenganisha Gaza na Israel pale kundi la wanamgambo wa Hamas wanaolidhibiti eneo hilo la Gaza lilipotangaza mgomo jumla, shule na taasisi za serikali zimefungwa ili watu wengi zaidi washiriki katika maandamano ya leo .

Maafisa wa huduma za afya wamesema watu 30 wamejeruhiwa katika mapambano hayo yaliyoripuka wakati wa maandamano ya Nakba- yanayoitishwa kila may 15, kuikumbuka siku wapalastina walipolazimishwa kuyahama maskani yao na kuundwa taifa la Israel mwaka 1948.

Mashahidi wanasema wanajeshi wa Israel waliwafyetulia maji yaliyovunda na gesi za kutoa machozi waandamanaji waliokuwa wakipaza sauti kuwataka walowezi waondoke. Risasi za mpira pia zimetumika wanasema.

Msemaji wa polisi ya Israel amesema wafanyafujo wasiopungua 7000 waliandamana kariibu na uzio wa mpakani na kwamba jeshi lilibidi kuwatawanya.

Uzio unaoitenganisha Gaza na Israel
Uzio unaoitenganisha Gaza na IsraelPicha: Reuters/A. Cohen

Maandamano ya Naqba -"Balaa",yanadai wakimbizi wa Palastina warejee katika maskani yao ya jadi

Maandamano ya mwaka huu ya Naqba yanajiri wiki mbili baada ya makubaliano ya kuweka chini silaha kufikiwa kaati ya Hamas na Israel ili kumaliza mapigano makali yaliyodumu siku mbili. Mjumbe wa Qatari aliyesaidia kufikia makubaliano hayo ya kuweka chini silaha amewatolea wito Hamas wahakikishe maandamano ya leo haykithiri.

Kwa kipindi cha zaidi ya mwaka sasa wapalastina wanaoishi katika ukanda wa Gaza wamekuwa wakiandamana kila wiki katika eneo hilo la uzio. Wanadai haki ya kurejea  mamilioni ya wakimbizi wa kipalastina na vizazi vyao katika ardhi zao za jadi ambazo leo hii zinakaliwa na Israel pamoja pia na kusita kuzingirwa eneo hilo na Israel. Itafaa kusema kwamba Israel inalizingira eneo la Ukanda wa Gaza tangu miaka 12 iliyopita.

Kwa mujibu wa wizara ya afya ya eneo hilo linaloongozwa na Hamas, tangu maandamano ya kudai haki ya kurejea nyumbani wapalastina yalipoanza, wanajeshi wa Israel wameshawauwa waandamanaji 305 wa kipalastina, wakiwemo watoto 59 na wanawake 10.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/dpa/AP

Mhariri: Josephat Charo