1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMamlaka ya Palestina

UN: Vita vya Gaza vimewaathiri mno wanawake na watoto

17 Aprili 2024

Umoja wa Mataifa umetoa wito na kusema vita vya miezi sita huko Gaza vimesababisha vifo vya wanawake 10,000 wa Kipalestina ambao 6, 000 kati yao wamewaacha yatima karibu watoto 19,000.

https://p.dw.com/p/4esOO
Watoto wameathirika pakubwa na vita vya gaza yasema ripoti ya shirika la UNICEF
Watoto wameathirika pakubwa na vita vya gaza yasema ripoti ya shirika la UNICEFPicha: Mohammed Salem/REUTERS

Umoja wa Mataifa unaeleza kuwa wanawake hao hujikuta katika mazingira hatarishi kutokana na majukumu yao ya ulinzi, ustawi, lakini pia kutafuta chakula na maji kwa ajili ya familia zao.

Akitoa taarifa kutoka mjini Cairo kwa waandishi wa habari wa Umoja wa Mataifa mjini Geneva, Tess Ingram, mtaalamu wa mawasiliano katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) amesema:

"Katika kipindi cha miezi sita iliyopita, idadi kubwa ya watoto wamejeruhiwa katikati ya mashambulizi makali na mara nyingi ya kiholela. Maisha yao daima yamebadilika kutokana na ukatili wa vita. Jumla ya watoto waliojeruhiwa katika mzozo huu ni ngumu mno kutathminiwa, lakini takwimu za hivi punde kutoka kwa Wizara ya Afya ya Palestina inakadiria kuwa zaidi ya watoto 12,000 wamejeruhiwa, ambao ni sawa na takriban watoto 70 wanaojeruhiwa kwa siku huko Gaza tangu kuanza kwa mzozo huu.", alisema Ingram.

Wizara ya Afya ya Gaza imetangaza hii leo kuwa jumla ya watu 33,899 wameuawa na wengine 76,664 wamejeruhiwa huko Gaza.