1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani na Kenya zatambua dhima ya UN

21 Januari 2026

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani anazitembelea Kenya na Ethiopia, wakati siasa ya ulimwengu ikiendeshwa kwa shinikizo la rais wa Marekani Donald Trump ambaye anatishia uhai wa Umoja wa Mataifa

https://p.dw.com/p/57CDK
Waziri wa mambo ya kigeni wa Kenya  Musalia Mudavadi na wa Ujerumani Johann Wadephul wakiwa mjini Nairobi
Waziri wa mambo ya kigeni wa Kenya Musalia Mudavadi na wa Ujerumani Johann Wadephul wakiwa mjini Nairobi Picha: Sebastian Gollnow/dpa/picture alliance

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Johann Wadephul ameanza hivi leo ziara yake ya siku mbili katika kanda ya Afrika Mashariki, akizitembelea Kenya na Ethiopia.

Mwanadiplomasia huyo wa ngazi za juu wa Ujerumani ametilia mkazo umuhimu wa dhima ya Umoja wa Mataifa katika kuitatuwa migogoro ya ulimwengu huku ukiweko wasiwasi kwamba rais wa Marekani Donald Trump huenda anapanga kuunda chombo cha kukinzana  na Taasisi hiyo ya dunia.

Ujerumani yatoa wito wa mageuzi makubwa kwenye Baraza la Usalama la UN

Ametowa mtazamo huo pamoja na mwenzake wa Kenya Musalia Mudavadi walipokutana  mjini Nairobi. Wadephul  pia anakutana na rais William Ruto hivi leo.

Msimamo wa Ujerumani na Kenya kuhusu umuhimu wa  Umoja wa Mataifa umekuja chini ya kiwingu cha wasiwasi uliosababishwa na hatua ya Trump ya kuunda  bodi ya amani ambayo itawajibika kusimamia juhudi za ujenzi mpya wa eneo la Ukanda wa Gaza baada ya vita.