1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tillerson ziarani barani Afrika

Isaac Gamba
7 Machi 2018

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani Rex Tillerson anaanza ziara ya mataifa matano barani Afrika ikiwa ni ziara yake ya kwanza barani humo ambapo atakuwa na mazungumzo na viongozi kadha barani humo.

https://p.dw.com/p/2tkxO
Mexiko NAFTA-Verhandlungen | Rex Tillerson
Picha: Reuters/H. Romero

 Kama inavyoeleza taarifa ya mwandishi wa DW  Sella Oneko ziara hiyo ya Tillerson itamchukua hadi Chad, Djibouti, Ethiopia, Kenya na Nigeria ambapo mazungumzo yanatarajia kujikita katika kujadili jinsi ya kufanya kazi pamoja  kudhibiti ugaidi, kuboresha hali ya amani na usalama, masuala ya utawala bora pamoja na ushirikiano katika biashara na uwekezaji.

Aidha  Tillerson anatarajia kukutana na maafisa wa Marekani katika balozi za nchi hizo pamoja na maafisa wa Umoja wa  Afrika katika makao makauu ya umoja huo mjini Addis Ababa.

Ziara hii inakuja ikiwa ni zaidi ya mwezi mmoja tangu rais Donald Trump wa Marekani  alipowakasirisha baadhi ya viongozi wa Afrika alipotamka katika Ikulu ya Marekani ya White House kuwa asingetaka wahamiaji kutoka nchi alizoziita zilizovunda  hali iliyoupelekea Umoja wa Afrika kudai aombe radhi.

Hii ni ziara  ya kwanza  rasmi ya Tillerson barani Afrika ambapo Marekani inatarajia kuja na sera bayana kuhusu Afrika  licha ya maafisa wawili wa ngazi ya juu wa Marekani  Nikki Haley na Donald Yamamoto kuwa tayari wamezuru barani Afrika.

Akizungumza wakati wa kikao na waandishi wa habari katika kuelekea ziara hiyo ya Rex Tillerson barani Afrika Donald Yamamoto ambaye ni kaimu waziri wa mambo ya nje ya Marekani anayehusika na masuala ya Afrika alisema miongoni mwa nchi ambazo Tillerson atazuru ikiwa ni pamoja na Kenya, Ethiopia na Nigeria  zina mahusiano imara na Marekani  na pia zina ofisi za mashirika makubwa ya Umoja wa Mataifa na kimataifa.

Tillerson kuzuru pia Djibouti

Yamamoto ameongeza kuwa ziara ya Tillerson nchini Djibouti  ni suala lingine tofauti kutokana na Marekani  kuwa na kambi kubwa ya kijeshi nchini humo ambayo inaitumia katika kuratibu mapambano dhidi ya ugaidi katika pembe ya Afrika pamoja na operesheni dhidi ya ugaidi katika ghuba ya Aden.

Wakati Tillerson akitarajiwa kuzuru pia nchini Kenya suala linalohusiana na mkwamo wa kisiasa nchini humo kati ya serikali na upinzani linaiweka Marekani katika nafasi ngumu mnamo wakati kukiwa ni mipango ya kufanyika mazungumzo kati ya rais Uhuru Kenyatta, serikali na wawakilishi wa asasi za kiraia nchini humo.

Hata hivyo kaimu waziri  wa mambo ya nje wa Matrekani anayehusika na masuala ya Afrika Yamamoto aalikwepa kuzungumzia moja kwa moja iwapo  ujumbe wa Rex Tillerson utakutana na kambi ya upinzani inayoongozwa na Raila Odinga ingawa alisema kuwa  hawaupuuzi upinzani kwani yeye mwenyewe pamoja na balozi wa Marekani nchini Kenya tayari wamekwishakutana na Odinga  mara kadhaa na kusisitiza upinzani pia una mchango muhimu.

Äthiopien Ministerpräsident Hailemariam Desalegn
Hailemariam Desalegn -Waziri Mkuu wa Ethiopia aliyejiuzuluPicha: Getty Images/AFP/Z. Abubeker

Ziara ya Tillerson nchini Ethiopia inakuja mnamo wakati Ethiopia ikiwa katika mkwamo wa kisiasa uliotokana na mgogoro na maandamano yanayoendelea nchini humo hali iliyopeleka pia waziri mkuu  Haillemariam Desalegn kulazimika kujiuzulu.

Aidha Tillerson huenda akawa na mazungumzo na waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov nchini Ethiopia ambaye ameanza pia hapo jana ziara  barani Afrika ingawa haijathibitishwa rasmi iwapo ratiba itaruhusu kufanyika  mazungumzo hayo. Hiyo ikiwa ni kwa mujibu wa wizara ya mambo ya nje ya Urusi.

Mwandishi: Sella Oneko

Tafsiri: Isaac Gamba/dw

Mhariri :Mohammed Abdul-Rahman