1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bush aiunga mkono Ukraine kujiunga na NATO

Mtullya, Abdu Said1 Aprili 2008

Rais G.W Bush wa Mareekani anafanya ziara nchini Ukraine kwa madhumuni ya kuunga mkono ombi la nchi hiyo kujiunga na NATO.

https://p.dw.com/p/DYa7
Rais G W Bush akisalimiana na rais Yushenko wa Ukraine.Picha: AP



Rais George  W. Bush  wa  Marekani yupo nchini Ukraine  katika  ziara yenye lengo la kuiunga mkono nchi hiyo inayokusudia kujiunga na jumuiya ya kijeshi ya NATO.


Rais Bush anaefanya ziara nchini Ukraine  amesema  anaunga  mkono thabiti lengo la nchi hiyo la kuwa mwanachama wa mfungamano wa kijeshi -   NATO.  Rais Bush amesema ataweka   mkazo juu ya suala hilo kwenye mkutano  wa viongozi wa nchi za NATO utakaoanza   kesho mjini Bucarest Rumania. Amesema atawataka viongozi wengine wa NATO waunge mkono maombi ya Ukraine na  Georgia ya kujiunga NATO.

Wakati  huo huo  rais Bush  ameonya kuwa Urusi  haitakuwa na kura ya veto kwenye mkutano wa nchi  za NATO ambapo viongozi wa jumuiya hiyo ya kijeshi  wataamua juu ya kuwaingiza wanachama wapya.

Rais Bush ametoa kauli hiyo kufuatia onyo lililotolewa na Urusi juu ya Ukraine inayokusuddia kujiunga  na jumuiya ya NATO.Urusi imesema ikiwa Ukraine itajiunga na  NATO, hatua hiyo itasababisha  mgogoro  mkubwa  katika uhusiano baina ya nchi hiyo na Urusi.

Naibu waziri wa mambo ya nje wa Urusi Grigory Karasin amekaririwa na mashirika ya habari akisema,ikiwa Ukraine  itaingizwa  katika NATO,hatua hiyo itaathiri  usalama wa bara la Ulaya

Naibu waziri huyo amezitaka nchi  za magharibi  ziamue , ni aina gani ya uhusiano zinata uwepo baina yao na Urusi.

Hatahivyo rais Viktor Yushenko  wa Ukraine amesema nchi yake  inatumai kupata ishara nzuri kutoka kwa viongozi wa nchi za NATO  watakaokutana kuanzia kesho mjini Bucarest, Rumania.

Wadadisi wanasema  kauli ya rais Yushenko itasababisha mvutano zaidi baina ya Urusi na nchi za magharibi.

Viongozi  wa nchi  za  NATO wanatarajia kuamua juu ya uanachama wa Ukraine kwenye  mkutano wa wa  kesho mjini Bucarest.